• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Bandari ya Lamu kuanza kutumiwa kuingiza mafuta ya nazi

Bandari ya Lamu kuanza kutumiwa kuingiza mafuta ya nazi

Na KALUME KAZUNGU

BANDARI ya Lamu hivi karibuni itaanza kutumiwa kuingiza nchini mafuta ghafi ya nazi kutoka Indonesia.

Balozi wa Indonesia nchini Kenya, Bw Mohamad Hery Saripudin, amesema Indonesia itaanza kutumia bandari hiyo katika usafirishaji wa bidhaa kuingia na kutoka nchini Kenya, na miongoni mwa bidhaa kuu zitakazoingizwa ni mafuta hayo ya nazi.

Bw Saripidin alisema kwa miaka mingi Kenya na Indonesia wamefurahia uhusiano na ushirikiano mwema wa kibiashara, ambapo Kenya imekuwa ikipokea mafuta hayo kwa wingi pamoja na karatasi na bidhaa nyinginezo kutoka Indonesia.

Kwa upande mwingine, nchi hiyo huagiza bidhaa kama vile majani chai, kahawa na bidhaa za ngozi kutoka Kenya.

Akizungumza mwishoni mwa wiki alipozuru Lamu, aliahidi ataendelea kupigania ushirikiano huo wa kibiashara kudumu kati ya nchi hizo mbili.

“Tumezuru bandari ya Lamu ilikutathmini utendakazi wake na kuona na nafasi gani tutatumia ili kuendeleza biashara hapa bandarini. Kwa miaka mingi tumekuwa tukitumia bandari ya Mombasa kusafirisha mafuta ghafi ya nazi kutoka Indonesia hadi Kenya. Kwa sababu tuko na bandari ya Lamu, pia tutaitumia katika usafirishaji wa mafuta ghafi ya nazi kwa wingi,” akasema Bw Saripudin.

Meneja wa bandari hiyo, bw Salim Bunu, alitoa wito kwa wawekezaji wengine pia waende kutembelea bandari ili wajitafutie nafasi zinazoweza kukuza biashara zao kimataifa.

Bw Bunu alisema mbali na bandari ya Lamu, pia kuna mpango wa kuanzisha eneo la viwanda.

“Nashukuru kwa ziara ya balozi Saripudin. Ombi langu ni kwamba uwarai wawekezaji waje kutafuta mwanya wa kuwezeka viwanda hapa Lamu ili kuona kwmba shughuli za bandari ya Lamu zinafaulu hata zaidi,” akasema Bw Bunu.

Bandari ya Lamu ilifunguliwa rasmi na Rais Uhuru Kenyatta mnamo Mei 20 mwaka huu katika hafla iliyoshuhudia meli ya kwanza ya mizigo kwa jina, MV CAP Carmel ikitia nanga kwenye kiegesho cha kwanza cha Bandari ya Lamu eneo la Kililana.

Hatua hiyo iliashiria mwanzo rasmi wa shughuli za uchukuzi wa kibiashara bandarini humo.

Wakati wa hafla hiyo, Rais Kenyatta pia alitangaza kwamba ujenzi unaoendelea wa viegesho viwili vya Lapsset utakamilika ifikapo Oktoba 2021.

You can share this post!

AKILIMALI: Matumizi ya vitunguu kukabili kero ya wadudu...

Arsenal kumtia fowadi Alexandre Lacazette mnadani ndipo...