• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:55 AM
Danny Ings abanduka Southampton na kutua Aston Villa

Danny Ings abanduka Southampton na kutua Aston Villa

Na MASHIRIKA

ASTON Villa wamemsajili fowadi raia wa Uingereza, Danny Ings kutoka Southampton kwa mkataba wa miaka mitatu uliogharimu Sh3.9 bilioni.

Ings, 29, anakuwa mchezaji wan ne kuingia katika sajili rasmi ya Villa baada ya Leon Bailey, Emiliano Buendia na Ashley Young.

Hadi alipoagana na Southampton waliomsajili kutoka Liverpool mnamo 2018, Ings alikuwa amefungia ‘The Saints’ mabao 46 kutokana na mechi 100.

Ings ambaye alikuwa aingie katika mwaka wa mwisho wa mkataba wake na Southampton, alikataa ofa ya kutia saini kandarasi mpya ya miaka minne ambao ungemshuhudia akiwa mchezaji anayedumishwa kwa mshahara wa juu zaidi uwanjani St Mary’s.

Kampeni za Ings katika kikosi cha Liverpool kilichojivunia huduma zake kwa miaka minne zilitatizwa pakubwa na majeraha mabaya ya goti yaliyomweka nje kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Licha ya kuwa sehemu ya kikosi kilichotegemewa na kocha Gareth Southgate wa Uingereza kati ya Septemba na Oktoba, matumaini ya Ings kuwakilisha timu yake ya taifa kwenye fainali za Euro 2020 yalizimika ghafla baada ya kuambukizwa virusi vya corona.

Anatua sasa uwanjani Villa Park wakati ambapo kiungo raia wa Uingereza, Jack Grealish anakamilisha uhamisho wake hadi Manchester City kwa kima cha Sh15.6 bilioni.

Kocha Ralph Hasenhuttl wa Southampton amesema kwamba analenga sasa kutumia fedha ambazo zimetokana na kuuzwa kwa Ings kukisuka upya kikosi chake kwa ajili ya kampeni za msimu mpya wa 2021-22.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

World Rugby yapongeza Mkenya Humphrey Kayange kuingia...

NMS yafungua rasmi mradi wa maji uliokamilika sokoni...