• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:47 PM
Demokrasia imeshinda, asema Biden baada ya kuapishwa kuwa Rais

Demokrasia imeshinda, asema Biden baada ya kuapishwa kuwa Rais

CHARLES WASONGA NA MASHIRIKA

NI rasmi sasa kwamba Joe Biden ndiye Rais wa 46 wa Amerika baada ya kula kiapo cha afisi Jumatano, Januari 20, 2021, jijini Washington, Amerika.

“Demokrasia imeshinda,” alisema akihutubu baada ya kulishwa kiapo na Jaji Mkuu John Roberts.

Rais anayeondoka Donald Trump, ambaye hajakubali rasmi kushindwa na Bideni, hakuhudhuria sherehe hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Capitol Hill, Washington. Hata hivyo, makamu wa rais anayeondoka Mike Pence alihudhuria.

Trump ni rais wa kwanza kukosa kuhudhuria sherehe ya kuapishwa kwa rais mpya wa Amerika tangu mwaka wa 1896.

Rais huyo mpya ametangaza msururu wa maamuzi rasmi yanayolenga kubatilisha sera kadhaa kuu za Trump.

Makamu wa Rais mteule Kamala Harris ndiye aliyeapishwa kabla ya Biden, na kuwa mwanamke wa kwanza wa mweusi na wa asilia ya Asia-Amerika kuhudumu katika wadhifa huo wa pili kimamlaka kutoka wa urais.

Usalama uliimarishwa katika ndani na nje ya ukumbi ambako hafla hiyo iliendeshwa baada ya jengo hilo Januari 6 kuvamiwa na wafuasi wa Trump walioandamana kupinga uhalali wa ushindi wa Biden.

Zaidi ya maafisa 25, 000 wa usalama walimwagwa katika eneo la sherehe hiyo ambayo haikuhudhuriwa na maelfu ya wananchi kama ilivyo ada. Hii ni kutoka na janga la Covid-19.

Katika hotuba yake Biden alitaja siku hiyo kama ya “historia na matumaini”.

‘Roho yangu yote imejitolea kurejesha Amerika mahala ambapo ilikuwa zamani,” akaongeza.

Huku akitaja haja ya kuwepo kwa umoja baada ya utawala wa Trump uliojaa misukosuko mingi, Biden aliahidi kuwahudumia Waamerika wote- wakiwemo wale ambao hawakumpigia kura katika uchaguzi wa Novemba 3, 2020.

Miongoni mwa marais wa zamani wa Amerika waliohudhuria ni; Barack Obama, ambaye Bideni alihudumu chini yake kama Makamu Rais kwa miaka minane, Bill Clinton na George W Bush.

Wasanii Lady Gaga-ambaye aliimba wimbo wa kitaifa- na Jennifer Lopez na Garth Brooks waliongoa watu wachache waliohudhuria hafla hiyo ya kihistoria..

Majira ya asubuhi Jumatano, Bw Biden, 78, alihudhuria ibada ya shukrani katika Kanisa moja Katoliki Washington.

You can share this post!

Bobi Wine alia njaa majeshi yekiendelea kumfungia nyumbani...

Kibarua cha kurejesha hadhi ya Amerika duniani chaanza