• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Everton kuachilia Moise Kean kurejea Juventus kujaza pengo la Ronaldo

Everton kuachilia Moise Kean kurejea Juventus kujaza pengo la Ronaldo

Na MASHIRIKA

EVERTON wameanzisha mazungumzo na Juventus kuhusu uwezekano wa fowadi matata raia wa Italia, Moise Kean kujiunga upya na kikosi hicho cha kocha Massimiliano Allegri.

Haijabainika iwapo mpango huo utakuwa ni kwa mkopo au mkataba wa kudumu.

Kean, 21, angali na miaka mitatu katika mkataba wake wa miaka mitano na Everton. Alisajiliwa kutoka Juventus mnamo 2019 kwa kima cha Sh3.9 bilioni.

Sogora huyo amechezeshwa mara mbili na Everton msimu huu wa 2021-22 chini ya kocha Rafael Benitez japo alionyeshwa kadi nyekundu katika mechi ya League Cup dhidi ya Huddersfield Town mnamo Agosti 24, 2021.

Baada ya kufungia Everton mabao mawili pekee katika mechi 33 za msimu wa kwanza, Kean alitumwa kambini mwa Paris Saint-Germain (PSG) ya Ufaransa kwa mkopo. Akiwa huko, alipachika wavuni mabao 16 kutokana na mechi 36.

Juventus kwa sasa hawana fowadi tegemeo tangu Cristiano Ronaldo aagane nao na kurejea upya kambini mwa Manchester United ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Arsenal kutamatisha mkataba wa Willian anayetaka kurejea...

Tottenham wakomoa Watford na kudhibiti kilele cha jedwali...