• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 9:55 AM
FORT JESUS: Historia, utamaduni, utalii, sanaa na utafiti

FORT JESUS: Historia, utamaduni, utalii, sanaa na utafiti

NA RICHARD MAOSI

Ngome ya Fort Jesus inasifika kote ulimwenguni kutokana na muundo wake wa kipekee, mbali na kuchangia kwa uchumi wa wakazi wengi wa pwani pamoja na kutengeneza nafasi nyingi za ajira miongoni mwa vijana.

Hata hivyo jambo lisilofahamika kwa wageni wengi wanaotua Mombasa ni kuwa, Fort Jesus ilitengenezwa na Waswahili halisi wa mwambao wa pwani na kuchukua umbo la binadamu ukiangalia kutoka mbali.

Kulingana na hifadhi ya kumbukumbu, wapwani walipata udhibiti wa ngome hii mwaka wa 1741 kabla ya mwingereza kutwaa hatamu 1895 enzi za ukoloni kama Protectorate of Kenya.

Mnamo mwaka wa 2001 UNESCO ikatoa kibali kwa Fort Jesus kama World Heritage Site na kuibuka kama mojawapo ya minara bora duniani iliyowahi kutengenezwa na kuhifadhiwa kwa muda mrefu.

Kuanzia hapo ndio mnara unaopokea wageni wengi zaidi katika ukanda wa Pwani na jumuiya ya Afrika Mashariki, na siku hizi ni makavazi ya kuhifadhi vyombo vya kale, michoro na miundo mbalimbali ya zana za kivita.

Taifa Leo Dijitali ilipiga kambi kubaini umuhimu wa ngome ya Fort Jesus kwa wakazi wa Pwani, hasa ikizingatiwa kuwa ni sehemu yenye utajiri mkubwa kwa utamaduni wa pwani, kuanzia chakula, mavazi, ufinyanzi , nyimbo na mashairi.

Mabaki ya wanyama wa majini

Mabaki ya nyangumi wa kiume aina ya Humback whale mrefu zaidi ulimwenguni aliyewahi kuishi, mwenye futi 48, yamehifadhiwa katika ngome ya Fort Jesus Mombasa na ni kivutio kikubwa cha watalii wa kigeni kutoka bara Asia na Uropa.

Huyu ni kiumbe ambaye anapatikana katika takriban bahari zote ulimwenguni, na anafahamika kutokana na maumbile ya kumiliki nundu,pamoja na uwezo wake wa kuimba, nyimbo za kawaida.

Humback whale hujumuika na nyangumi wenzake kwa makundi wakati wa kuwinda na kutafuta chakula majini, huku wakinengua densi na kuwavutia watalii wengi wanaotembea pwani ya Kenya kufurahia, mbwembwe za samaki hawa ambao husafiri kilomita nyingi.

Kwa mujibu wa akailojia ya pwani inayochungza na kudadisi mabaki ya viumbe wa kale,mabaki ya humback whale yalipatikana mnamo 1992 katika ufuo wa bahari Hindi akiwa amefariki.

Mabaki yenyewe yalipatikana katika sehemu ya Ungwana Bay Kipini katika kaunti ya Tana River ingawa chanzo cha kifo chake hakikubainika moja kwa moja, mpka wa leo.

Inasemekana kuwa umri wa nyangumi wa sampuli hii unaweza kuwa baina ya miaka 19-24.

Nyumba ya kihistoria ya Omani

Disemba tarehe 13 1698 ni mahali hapa ambapo waomani walishinda wareno na kuikomboa ngome ya Fort Jesus,Hatimaye waomani walijitahidi na kuimarisha hadhi ya ngome kwa kuzirefusha kuta, kila upande ili kuikinga ngome dhidi ya mashambulizi ya adui.

Walichimba mahandaki ya kujificha pamoja na kisima cha kuteka maji ya kunywa ,wakati wa kipindi cha muingereza 1980 nyumba hii ilirekebishwa na kufanywa kituo cha maonyesho.

Baadaye 2017 wizara ya michezo kupitia wizara ya Usultani wa Uomani walirekebisha na kuendeleza sehemu maalum kuwa ukumbi wa maonyesho, kwa watalii na wenyeji.

Hii iliwasaidia vijana wenge wanaofanya kazi za sanaa kujipatia ajira kama waelekezaji na walimu wa historia ndefu ya wapwani hususan Waswahili.

Sanaa

Taifa Leo Dijitali ilikutana na kijana Fadhili Swaleh ambaye ni mchoraji mahiri wa vibonzo na mabango ya kubandika ukutani, na amekuwa akifanya kazi hii tangu mwaka wa 2014.

Anasema alianza kazi yenyewe alipogundua alikuwa na kipaji cha kuchora na kuibua picha ya hali halisi ya mtu wa kawaida kwa watalii na wenyeji wa pwani ambao humiminika mara kwa mara katika Ngome ya Fort Jesus.

Yaonekana kazi yake inaendelea kupata mashiko kutokana na idadi kubwa ya wageni wanaosimama katika kibanda chake kufurahia kazi yake ya ubunifu, wengi wao wakiwa ni wanafunzi wa shule za msingi na upili.

Aidha amekuwa mchoraji wa kazi za nyumbani na hata kwenye matatu akiamini kuwa kipaji kama kazi nyingineyo kinalipa muradi tu msanii ajue kuwasilisha ujumbe wake kwa umma.

Alisema kuwa yeye hutumia kalamu ya wino, makaratasi, rangi ya majimaji na ile ya kupaka ukutani akiwa katika karakana yake.

Aliongezea kuwa mnara huo uliotengenezwa baina ya 1593 -1596 na wareno una historia pana ambapo ulilenga kuwakinga wareno dhidi ya maadui wakati wa kivita.

Hatimaye Fort Jesus iliingia katika orodha ya turadhi za kitaiifa manamo 2001 kupitia UNESCO World Heritage Committe.

Msanii anaweza kuibua michoro ya kuhamasisha, kuburudisha na kuzindua kwa sababu mara nyingi anatumia malighafi kutoka kwenye mazingira ya jamii halisia kama vile vipande vya miti mashina na kadhalika.

Utafiti

Katika mahojiano yake na Runinga ya NTV Fatma Twahir, mtaalamu wa miundo misingi anasema ngome ya Fort Jesus imekuwa ikisimama kwa miaka 420 bila kitu chochote kubadilika.

Anasema ni kumbukumbu ya kujivunia kwa sababu wakati wa shule wanafunzi wengi hufika hapa kujifundisha mambo mengi hasa yale yanayohusiana na somo la historia, Jiografia na somo la Kiswahili.

Anasema kuwa wamekuwa wakishirikiana na jamii ya waswahili kuwasaidia kufanya kazi ndani ya ngome kwa kuwafundisha namna ya kuwaelekeza wageni.

Alieleza kuwa kuna walimu wanaowafundisha wenyeji mambo ya ekolojia ya kisayansi ili waweze kuwa na njia ya kupambanua mambo yanahohitaji maelezo ya kitaaluma.

Aidha wamekuwa wakiwafundisha utamaduni wa jamii zingine kama vile Omani kwa kufananisha maisha yao ya kale na yale ya kisasa ambapo utandawazi umekuja na mabadiliko mengi kwa kizazi cha leo.

Wasomi vilevile wamekuwa wakipata nafasi ya kuendeleza taaluma zao katika kiwango cha juu kama vile shahada ya uzamili na uzamifu , hususan wale wanaojikita katika maswala na turadhi za waswahili.

Vilevile wanafunzi wanaosomea taaluma za Hospitality wamekuwa wakipata fursa ya kufanya majaribio baada ya kutimiza kozi zao katika ngome ya Fort Jesus.

“Maeneo mengine ya kuvutia ni kama vile Shimoni walipohifadhiwa waumwa, Jumba la Mtwana, Gedi na Rabai ,”akasema.

Alieleza kuwa ni ngome ambayo imedumu licha ya nyakati mbalimbali kubadilika kuanzia enzi za wakoloni mpaka kizazi cha leo.

Ombi

Joy Mwangeka muuzaji wa shanga katika ngome ya Fort Jesus anasema ni sehemu inayofaa kuboreshwa ili isipoteza thamani yake kwa wakazi wa pwani kwa ujumla.

Akiwa mfanyibiashara anaona kuwa serikali ya kaunti inaweza kupaka rangi na kuziba baadhi ya nyufa ambazo zimeanza kutokea katika sehemu za mjengo huu wa kale.

“Ingawa Fort Jesus inatoa taswira nzuri ukiangalia bahari na upepo mtulivu, vijana wengi bado sio wabunifu vya kutosha kujifaidisha na ngome hii,”akasema.

Alieleza kuwa utalii katika Pwani ya Kenya umekuwa ukiwasaidia wakazi wengi kupigana na janga la umaskini, hasa kwa mapato ya nje kuinua uchumi wa kitaifa.

You can share this post!

Jinsi ving’ora vilivyochanganya wakazi

Mahakama yaombwa iapishe majaji 41

adminleo