• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 12:46 PM
Jaramogi ahusishwa na mzozo wa mpakani

Jaramogi ahusishwa na mzozo wa mpakani

TOM MATOKE na WYCLIFF KIPSANG

MZOZO wa mpaka kati ya Kaunti za Nandi na Kisumu ulichukua mwelekeo mpya Jumatatu baada ya jina la aliyekuwa makamu wa rais Jaramogi Oginga Odinga kutajwa.

Viongozi kutoka Kaunti ya Nandi walisema kaunti hizo mbili zilibuniwa Jaramogi alipokuwa makamu wa rais wa rais wa kwanza wa Kenya Mzee Jomo Kenyatta.

Viongozi hao wakiongozwa na aliyekuwa mwenyekiti wa lililokuwa baraza la mji wa Nandi Charles Tanui walidai kwamba Jaramogi alimuomba Mzee Kenyatta kuruhusu watu wa jamii ya Waluo waliokuwa wakiishi Kisumu kuhama na kuishi maeneo ya milimani ya Nandi msimu wa mvua kubwa ili wasisombwe na mafuriko.

Walisema Mzee Kenyatta alikubali ombi hilo na mamia ya watu kutoka Nyanza waliruhusiwa kuishi Nandi karibu na mpaka kwa muda hadi mvua ipungue.

“Wakati Jaramogi aliacha kazi ya makamu wa rais, wenzetu kutoka Kisumu waliendelea kuishi katika ardhi ndani ya Kaunti ya Nandi hadi Mzee Kenyatta alipokufa 1978,” alisema Bw Tanui.

Viongozi wa Kaunti ya Nandi wameunga mipango ya Gavana Stephen Sang mpaka huo uchunguzwe upya. Bw Sang na viongozi hao wanataka maeneobunge ya Muhoroni na Kisumu Mashariki wakisema yalitwaliwa wakati wa ujenzi wa reli.

Wanadai kwamba Waingereza waliwafukuza Wanandi kwa sababu ya kupinga ujenzi wa reli. Bw Sang aliongoza mkutano wa viongozi wa Nandi miezi mitatu iliyopita kabla ya Tume ya Ardhi kuzuru eneo hilo.

Mkutano huo ulipitisha azimio la kuhakikisha maeneo yanayozozaniwa yamerejeshwa Kaunti ya Nandi. Walitaja maeneo hayo kama miji ya Miwani, Kibos, Kibigori, Kopere, Chemelil, Fort Tenan na Muhoroni. Hatua hiyo ilizua taharuki kwenye mpaka wa kaunti hizo mbili na kuathiri uwekezaji katika kilimo.

You can share this post!

Karua atakiwa kushirikiana na Waiguru

Ziara ya Moi yawakera wandani wa Ruto

adminleo