• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 4:31 PM
Marufuku dhidi ya Ngii yabatilishwa, sasa atawakilisha Kenya matembezi ya 20km kwenye Olimpiki

Marufuku dhidi ya Ngii yabatilishwa, sasa atawakilisha Kenya matembezi ya 20km kwenye Olimpiki

Na GEOFFREY ANENE

KENYA imefanikiwa katika rufaa yake dhidi ya mwanariadha wa metembezi ya kilomita 20, Emily Ngii kupigwa marufuku kushiriki Olimpiki mjini Tokyo, Japan.

Bingwa huyo wa mashindano ya African Games mwaka 2019 alimaliza wa kwanza katika mashindano ya kitaifa ya kuingia Olimpiki mnamo Juni 18 kwa saa 1:30:56 ugani Kasarani.

Muda wa kufuzu kushiriki matembezi ya kilomita 20 ni 1:31:00.

“Tulikata rufaa dhidi ya marufuku hiyo mnamo Juni 18. Alikuwa ameonyeshwa kadi nyekundu na majaji mawili wa riadha za matembezi. Majaji walisikiliza rufaa yetu hiyo mapema Juni 19 na kuamua kuwa hakustahili kuonyeshwa kadi hizo nyekundu,” alisema kocha maarufu wa fani hiyo, George Kariuki katika mahojiano.

Ngii alijumuishwa katika kikosi cha wanariadha 43 ambacho Kenya imechagua Juni 19 kupeperusha bendera mjini Tokyo. Inamaanisha kuwa Kenya itakuwa na watembeaji wawili katika Olimpiki za 2020.

Samuel Gathimba alijikatia tiketi baada ya kukamilisha matembezi ya wanaume kwa saa 1:18:23. Alivunja rekodi yake ya kitaifa ya 1:19:04 aliyoweka kwenye mashindano ya kuchagua timu ya michezo ya Jumuiya ya Madola 2018.

Gathimba alizoa medali ya shaba kwenye michezo hiyo iliyoandaliwa mjini Gold Coast, Australia baada ya kumaliza nyuma ya mwenyeji Dane Bird-Smith (1:19:34) na Muingereza Tom Bosworth (1:19:38).

You can share this post!

Homeboyz yalimwa winga wake David Odhiambo akitawazwa...

Sonia: Chipukizi anayelenga nyayo za Priyank Chopra