• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
Mipasuko UDA na Jubilee yaibua vyama vipya Mlimani

Mipasuko UDA na Jubilee yaibua vyama vipya Mlimani

Na GITONGA MARETE

KUPOROMOKA kwa chama cha Jubilee na mng’ang’anio wa tiketi katika chama kipya cha United Democratic Alliance (UDA) ndizo sababu kuu zinazowasukuma wanasiasa kutoka eneo la Mlima Kenya kuunda vyama vidogo kuelekea uchaguzi mkuu ujao.

Ili kujihisi salama, wanasiasa kadhaa wanaogura chama tawala wanaamua kuunda vyama vipya ili walinde nafasi zao katika ulingo wa siasa hapo mwakani.

Mwanasiasa mkuu wa hivi punde kuunda chama kipya ni Gavana wa Meru Kiraitu Murungi ambaye alishinda kiti cha ugavana katika uchaguzi wa 2017 kwa tiketi ya Jubilee.

Ameunda chama cha Devolution Empowerment Party ambacho sasa kimejiunga na orodha ndefu ya vyama vidogo katika eneo la Mlima Kenya, iliyokuwa ngome ya Jubilee.

Vyama vingine vyenye mizizi katika eneo hilo ni Usawa Party kinachohusishwa na Gavana wa Murang’a Mwangi Wa Iria, Chama cha Kazi (CCK) cha Mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria na The Service Party (TSP) kinachoongozwa na aliyekuwa Waziri wa Kilimo Mwangi Kiunjuri.

Vyama vingine ni pamoja na; Party of National Unity (PNU) kinachohusishwa na Waziri wa Kilimo Peter Munya, Narc- Kenya cha Martha Karua, Tujibebe Wakenya Party kilichoundwa na aliyekuwa Gavana wa Kiambu William Kabogo na The New Democratic kilichoasisiwa na mfanyabiashara wa Nyeri Thuo Mathenge.

Vyama hivyo vimekubalika katika eneo la Mlima Kenya haswa baada ya Bw Kiunjuri, Bw Kuria na Bi Karua kuunda vuguvugu la Muungano wa Mlima Kenya.Mnamo Septemba mwaka huu, viongozi wa Jubilee walikutana na Bw Kiunjuri na Bi Karua katika mkahawa wa Serena, Nairobi ambako ilidaiwa walijadili mikakati ya kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022.

Wanasiasa wako mbioni kukumbatia vyama hivyo vidogo kutokana na imani kuwa baada ya Jubilee kupoteza ushawishi eneo la Mlima Kenya, itakuwa vigumu kwa mwanasiasa kushinda kiti katika uchaguzi huo kwa kutumia tiketi yake.

Gavana Murungi, ambaye ametangaza kuwa “Jubilee imekufa na kuzikwa” alitwaa chama cha Restore and Build Kenya (RBK) na kugeuza jina lake kuwa DEP. RBK ilitumiwa na aliyekuwa Katibu katika Wizara ya Elimu Profesa James Ole Kiyiapi kugombea urais 2013.

Chama cha DEP kinatarajiwa kuchota umaarufu katika eneo la Mlima Kenya Mashariki linalojumuisha kaunti za Meru, Embu na Tharaka Nithi.

Bw Murungi ambaye juzi alisema “mwanasiasa yeyote ambaye anataka kupoteza katika uchaguzi mkuu wa 2022 awanie kwa tiketi ya Jubilee” ameibuka kuwa mfalme wa kuunda vyama vipya baada ya kupata idhini ya kutwa chama cha RBK.

Tayari Msajili wa Vyama vya Kisiasa Anne Nderitu ameidhinisha jina jipya la DEP na alama ya Basi. Alama hiyo ndiyo ilikuwa ya chama cha Alliance Party of Kenya (APK) ambacho Bw Murungi alitumia kuwania ugavana wa Meru 2013 na kushinda.

Ni miongoni mwa vyama 13 vilivyovunjwa mnamo 2016 ili kuunda chama tawala cha Jubilee ambacho sasa kimesalia kigae.

Hii ni baada ya Naibu Rais William Ruto kuongoza kukiasi na kuunda cha cha UDA, Rais Uhuru Kenyatta aliporidhiana na kiongozi wa ODM Raila Odinga mnamo 2018.

Bw Murungi alisema kuwa eneo la Mlima Kenya Mashariki litatumia chama hicho cha DEP kujadiliana na vyama vya ODM, ANC, Wiper na KANU kuhusu ugavi wa rasilimali za kitaifa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022.

You can share this post!

Wafalme wa kuhadaa vijana

LEONARD ONYANGO: Siku ya Utamaduni ilifaa kuadhimishwa...