• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:05 AM
Pep Guardiola akiri kwamba Jurgen Klopp amemfanya kuwa kocha bora zaidi

Pep Guardiola akiri kwamba Jurgen Klopp amemfanya kuwa kocha bora zaidi

Na MASHIRIKA

PEP Guardiola wa Manchester City amesema uhasama mkubwa kati yake na Jurgen Klopp wa Liverpool katika ulingo wa ukufunzi umemfanya kuwa “kocha bora”.

Ni pengo la alama moja pekee ndilo linawaweka Man-City ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) nyuma ya Liverpool ambao ni viongozi wa jedwali la kipute hicho kufikia sasa msimu huu.

Liverpool watakuwa wenyeji wa Man-City uwanjani Anfield mnamo Jumapili ya Oktoba 3, 2021. Mara ya pekee ambapo Man-City walikosa kunyanyua taji la EPL chini ya kipindi cha miaka minne iliyopita ni wakati Liverpool walipotawazwa mabingwa mnamo 2019-20.

“Tangu nitue hapa Uingereza – na si katika mwaka wangu wa kwanza – Liverpool wamekuwepo huku juu kwenye soka ya EPL,” akasema Guardiola. Guardiola ambaye ni raia wa Uhispania, alipokezwa mikoba ya Man-City mnamo Julai 2016 huku Klopp akianza kuwatia makali masogora wa Liverpool mnamo Oktoba 2015.

Kabla ya hapo, wakufunzi hao wawili waliwahi kukabiliana katika Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga) wakati Guardiola alipokuwa akiwanoa Bayern Munich naye Klopp akiongoza kikosi cha Borussia Dortmund.

Guardiola amepoteza mechi nane dhidi ya Klopp katika mashindano yote, idadi hiyo ikiwa kubwa zaidi kuliko mkufunzi yeyote mwingine mpinzani wake.

 “Vikosi vinavyonolewa na Klopp vilinisaidia kuwa kocha bora,” akasema Guardiola atakayeongoza Man-City kuvaana na Liverpool ugenini siku chache baada ya kuwapiga Chelsea ligini kisha kutandikwa na Paris Saint-Germain (PSG) kwenye Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).

“Klopp aliniweka katika kiwango tofauti na cha juu kabisa katika ulingo wa ukufunzi. Aliniweka katika ulazima wa kufikiri sana na kunichochea kujituma zaidi kudhihirisha ukubwa wa uwezo wangu.

Hayo yote yalichangia ubora wangu na akanidumisha katika kazi hii yenye panda-shuka tele,” akasema Guardiola. “Kwa miaka minne iliyopita, Liverpool na Man-City wamekuwa wakiwania nafasi mbili za kwanza kwenye jedwali la EPL.

Ni ishara ya ubora wa kila kocha na ukubwa wa ushindani kati ya timu hizo mbili. Lakini EPL si ya vikosi viwili. Kuna timu nyinginezo zilizo na uwezo wa kupigania ufalme wa kipute hicho,” akaeleza.

Mnamo Februari 2021, Liverpool walipigwa na Man-City 4-1 katika EPL ugani Anfield na Klopp amekiri kwamba masogora wake watakuwa na kiu ya kulipiza kisasi.

“Hii ni mechi spesheli sana kila msimu. Lazima uwe na masogora wako wote na kila mmoja awe katika fomu nzuri ndipo kocha apate nafasi ya kumbwaga mwenzake,” akasema Klopp.

“Pengine Man-City kwa sasa ndicho kikosi bora zaidi barani Ulaya kwa sasa. Walicheza dhidi ya Chelsea wikendi iliyopita na wakashinda wakati ambapo kila mmoja alikuwa akitazamia Chelsea washinde kutokana na uthabiti wao wa sasa.

Lakini mambo yalikwenda kinyume kwa sababu Man-City walicheza soka safi.” “Lazima tushinde mechi hiyo dhidi ya Man-City kwa kufunga mabao na pia kubana safu ya ulinzi ipasavyo,” akasema Klopp.

  • Tags

You can share this post!

Matarajio makubwa ya mashabiki kutoka kwa Chelsea yanatutia...

Stoke City wakomesha rekodi ya kutoshindwa kwa West Brom...