Matatizo mengine yanayokumba sekta ya elimu jinsi yalivyoanishwa katika ripoti hiyo ni idadi ndogo ya walimu, ukosefu wa nidhamu kazini na baadhi yao kulemewa kabisa kuelewa teknolojia mpya inayotumika katika mafunzo shuleni. Hata hivyo, kinachosikitisha sana ni, kati ya walimu wanne, mmoja ana matatizo ya kiakili na husaka huduma za matibabu kwenye hospitali mbalimbali.
“Tume imetambua kwamba idadi ya walimu ambao wanaandamwa na matatizo ya kiakili inaendelea kupanda na kutatiza utekelezaji wa mtaala. Kwa hivyo, TSC imekuwa ikiendeleza hamasisho kwa kushirikiana na wadau wa sekta nyingine kuwaelimisha walimu kuhusu afya ya kiakili,” ikasema ripoti hiyo.
“Pia walimu wameboreshewa mpango wa bima ya afya ili kuwasaidia kwenye visa hivi vya afya ya kiakili,” ikaongeza ripoti hiyo.
Walimu hutumia bima ya afya kutoka kampuni ya Minet Kenya. Mwaka jana, TSC ilikuwa na walimu 346,000 ambayo inawalipa mishahara kando na wafanyakazi wake kwenye afisi zake mbalimbali nchini. Mwaka huu, walimu 10,000 wameajiriwa kando na wengine 20,000 ambao wapo mafunzoni na hawajapokezwa bima ya afya.
Mwezi uliopita, TSC ilichapisha majina ya walimu 36 ambao waliondolewa kwenye sajili yake. Mnamo Oktoba 2022, walimu 44 waliondolewa kwenye sajili hiyo huku wengine 73 wakitolewa mnamo Julai kutokana na sababu mbalimbali za ukosefu wa nidhamu. Kwenye ripoti hiyo, TSC pia imeyataja baadhi ya maeneo yanayokumbwa na utovu wa usalama kama ambayo hayana mazingira mazuri ya kufanya kazi.
Pia orodha hiyo inajumuisha maeneo kame ambapo walimu hukumbana na matatizo mbalimbali. Kwa hivyo, ripoti hiyo inaipendekezea serikali ishughulikie utovu wa usalama kwenye maeneo hayo hasa yale ambako wizi wa mifugo na visa vya ugaidi vimekithiri. Pia TSC inataka mgao zaidi ili kuwaongezea marupurupu walimu wanaofanya kazi katika maeneo hayo.