• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
VALENTINE OBARA: Ahadi ya kusafisha maji ya bahari imeisha ladha

VALENTINE OBARA: Ahadi ya kusafisha maji ya bahari imeisha ladha

NA VALENTINE OBARA

KWA muda mrefu sasa, wakazi wa kaunti za Pwani wamekuwa wakiahidiwa kusafishiwa maji ya baharini ili kuyatumia nyumbani.

Kaunti sita za Pwani ni baadhi ya maeneo nchini ambayo hukumbwa na uhaba mkubwa wa maji safi.

Wengi hulazimika kutegemea wahisani wanaowasambazia maji mitaani, kujichimbia visima kwa gharama kubwa au kununua maji wasiyojua yanakotoka.

Ingawa baadhi ya serikali za kaunti kwa ushirikiano na serikali ya kitaifa zimejaribu kuweka mikakati ya kuboresha hali hii, bado kuna tatizo kubwa kwa kuwa, maelfu ya wakazi wangali hutatizika kupata maji safi nyumbani kwao.

Ahadi ya kutatua hali hii kupitia kwa usafishaji wa maji ya baharini hasa katika kaunti zilizopakana na Bahari Hindi, imekuwa kama wimbo kwa miaka na mikaka.

Hakika, usafishaji wa maji ya baharini ili yatumiwe nyumbani ni jambo ambalo linawezekana. Kuna mataifa ulimwenguni ambayo yamedhihirisha uwezekano huu, hasa mataifa ya Uarabuni na kaskazini mwa Afrika.

Humu nchini, Wapwani wamekuwa wakipewa matumaini tele ila mpango huo mzima haujatimizwa wala kukaribia kuanzishwa.

Kumekuwa hata na wawekezaji ambao wamewahi kuzuru sehemu tofauti na kubadilishana mawazo na viongozi kuhusu kinachohitajika kufanywa lakini baada ya mazungumzo, hakuna hatua za kuridhisha hupigwa.

Wakati huu, wiki chache kabla kuandaliwa kwa uchaguzi mkuu, hatutaki kuendelea kupewa ahadi hizi zisizo na msingi.

Wagombeaji viti, hasa wa ugavana, wanafaa kwanza watueleze kwa nini wazo hili halijafanikiwa katika miaka iliyopita.

Hivyo basi, wanasiasa wasitoe tu ahadi kwamba, watasafisha maji ya baharini bali waeleze kwa mapana kile wanachonuia kufanya kufanikisha mpango huu.

Bila shaka, huu ni mpango ambao utahitaji rasilimali tele, hasa kifedha, kwa hivyo tuambiwe hizo pesa zitatoka wapi.

Ripoti za kimataifa huonyesha kuwa, miradi ya kusafisha maji ya baharini ili yatumiwe nyumbani huhitaji kiwango kikubwa mno cha kawi.

Baadhi ya mataifa ambayo yamewekeza katika miradi aina hii, huwekeza pia kwa uzalishaji wa kawi ya miale ya jua ili miradi hiyo isitatizike na usambazaji wa umeme, mbali na kupunguza gharama za kawi ya kawaida.

Kuna pia masuala mengi kuhusu athari za miradi aina hii kwa mazingira ya baharini, ambayo ni lazima yafafanuliwe na wanasiasa wanaotoa ahadi hizi kwa wananchi.

Wengi wa wanasiasa ambao hutoa ahadi za kusafisha maji ya baharini kwa matumizi ya nyumbani ni watu ambao wamewahi kuwa mamlakani katika vyeo tofauti au wamekuwa wandani wa wakuu wa kaunti.

  • Tags

You can share this post!

Ruto anamhemesha Raila hapa Pwani, Kingi asema

Mwalimu kizimbani kwa kumnajisi mwanafunzi

T L