JUMLA ya watu 4,104 wamekufa kutokana na ajali za barabarani nchini Kenya kufikia mwezi huu wa Novemba, kulingana na takwimu za hivi punde kutoka kwa Mamlaka ya Kitaifa kuhusu Usalama wa Barabarani (NTSA).
Idadi hii inawakilisha ongezeko la asilimia nne ya vifo barabarani ikilinganishwa na wakati kama huu mwaka jana ambapo jumla ya watu 3,947 waliangamia kupitia ajali hizo.
Lakini ili kupunguza ajali za kila mara za barabara mnamo Novemba 16, 2016, Rais mstaafu Uhuru Kenyatta alitangaza kuwa serikali ingetekeleza mpango ambapo madereva na makondakta wa matatu wangekuwa wakipokea mafunzo maalum katika Shirika la Vijana kwa Huduma za Kitaifa (NYS).
Alipokuwa akiongea katika kongamano la kitaifa la wajumbe wa chama cha wamiliki wa matatu (MOA) katika jumba la KICC, Nairobi, Kenyatta alisema mpango huo ungechangia katika kupunguzwa kwa ajali za barabarani.
Lakini hadi Septemba 13, 2022 alipoondoka mamlakani, serikali na MOA hazikuwa zimetekeleza mpango huo ilhali visa vya ajali za barabarani vimekuwa vikishuhudiwa kila mara, magari ya matatu yakihusika kwa wingi.
Mwenyekiti wa MOA Simon Kimutai na Waziri wa Uchukuzi Kipchumba Murkomen wakumbuke kutekeleze mpango huu wa 2016, ili kupunguza ajali za barabarani wakati huu ambapo msimu wa sherehe unabisha hodi.