NA KALUME KAZUNGU
KATIKA miji mingi mikubwa nchini, wafanyabiashara wa uchukuzi wa umma hurembesha sana vyombo vyao vya uchukuzi.
Vyombo hivyo vinavyojumuisha matatu, mabasi, tuktuk na pikipiki hupambwa kwa njia mbalimbali hasa kwa michoro na maandishi.Haya hufanywa kwa vile huwa inaaminika mapambo huvutia wateja kushinda kile ambacho hakijarembeshwa.
Imani hii imewasukuma wamiliki wa punda katika Kaunti ya Lamu pia kuamua kurembesha wanyama hao ambao hutegemewa sana kwa uchukuzi katika maeneo mbalimbali ya mji huo wa kale tangu jadi.
Kando na kugeukia ubunifu huo wa kuwarembesha punda wao kuwavutia watalii, wageni na hata wenyeji, imebainika ubunifu huo pia umeanza kuvutia wanasiasa ambao wanapamba punda kwa nembo zao katika msimu huu wa kampeni.
Unapotembea kwenye vishoroba vya mji wa Lamu, si ajabu kumpata punda akiwa amevalishwa mavazi ya rangi ya kuvutia, herini, shanga, kofia au hata kupakwa rangi mdomoni, kwenye kope na hata kwato, ilmradi uvutiwe kumkodi mnyama huyo.
Wahudumu waliohojiwa na Taifa Leo walibainisha kuwa, watalii huwa wanakodi punda wa kawaida ili kujivinjari kisiwani Lamu.
Wao hulipishwa ada tofauti kulingana na muda ambao wanataka kumtumia punda huyo.Bw Mohamed Omar ambaye ni mmiliki wa punda kisiwani Lamu, alisema wakati wa msimu mkuu wa utalii, yeye hupata hadi Sh2,000 kwa siku kupitia juhudi zake za kumrembesha punda na kumkodi kwa watalii kisiwani.
“Hapa ilibidi kuibuka na ubunifu huu wa kurembesha punda wetu ili kupata biashara. Watalii wamekuwa wachache kutokana na hali ya kiusalama eneo hili na pia janga la corona. Badala ya kutegemea biashara ya kubeba mizigo ambayo pia imepungua, ilibidi kutafuta jinsi tutawavutia hawa watalii kukodi punda wetu. Nashukuru kwamba kwa sasa biashara inanoga. Angalau tunapata mtaji wa kukimu familia zetu,” akasema Bw Omar.
Mmiliki mwingine, Bw Fadhil Abbas, aliye katika mtaa wa Mkomani mjini Lamu, anasema mbali na kuwavutia watalii, ni kupitia kuwapamba punda ambapo pia amekuwa akijizolea zawadi kutoka kwa wahisani na mashirika mbalimbali ya kutetea haki za wanyama.
Mnamo Mei 8, 2018 wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Punda Ulimwenguni, Bw Abbas alituzwa kwa kuibuka mmiliki wa punda mwenye tajiriba bora zaidi ya kumrembesha na kumtunza punda.
“Urafiki niliojenga na punda wangu umeniwezesha kupokea zawadi kochokocho kutoka kwa wahisani na mashirika. Mimi humpamba punda wangu vizuri na ukimuona utadhani ni binti mrembo. Tunashauriwa kumtunza punda ili atutunze. Hilo nimelidhihirisha mwenyewe kwani urafiki nilio nao na punda wangu umewasukuma watalii kutaka kumpanda punda huyo, hivyo napata fedha,” akasema Bw Abbas.
Kwa wengine wao, msimu wa siasa umeanza kuwaletea baraka kwani wanalipwa kuvisha punda wao nembo za wanasiasa mbalimbali.
Bw Yusuf Hamza anasema ni kupitia mbinu ya kuwapamba punda wao ambapo wanasiasa wametambua wanaweza kukodisha punda kupiga kampeni, hasa wakati wa mikutano ya hadhara na wanapofanya misafara mjini Lamu.
Kulingana na Bw Hamza, mara nyingi wao hubahatika kupokea ada za mapema kutoka kwa wanasiasa na vyama vyao, ambapo huwaagiza kuwapamba punda wao kwa rangi za vyama, hivyo kujipatia malipo ya juu.
“Wengi bila shaka wamejionea wanasiasa kama vile Raila Odinga wa ODM na Naibu wa Rais, William Ruto wa UDA wakiwa juu ya punda kila wanapofika hapa Lamu kuendeleza kampeni zao. Ukitazama barabarani wakati wa kampeni hizo, pia utawaona punda wakiwa wamerembeshwa kwa mavazi ya rangi ya chungwa kwa ODM au kijani na manjano kwa UDA.
“Hapo huwa hatufanyi bure. Huwa tumepokea malipo kutoka kwa wanasiasa na wenye vyama. Wanasiasa wengine ambao ni wafuasi pia huamua kututuza wanapoona rangi zao kwa punda wetu,” akasema Bw Hamza.
Abdallah Bakari, mkazi wa Langoni anasema mbali na biashara, mbinu ya kuwarembesha punda wao pia ni mojawapo ya kuonyesha upendo na shukrani kwa wanyama hao.
Kando na urembo, Taifa Leo pia ilibaini kuwa baadhi ya wakazi wamejikaza kuwafundisha punda wao lugha, hivyo husikilizana kimawasiliano.
Hatua hiyo pia imevutia pakubwa watalii na wageni wanaotembelea mji wa kale wa Lamu kujionea vimbwanga hivyo.Bw Mohamed Abeid ni mmoja wa wakazi wa kisiwa cha Lamu ambaye anadai kujipatia mtaji kupitia maonyesho ya punda wake ambao huwasiliana nao na hata kutii masharti anayotoa kwa wanyama hao.
“Mimi punda wangu huwapiga pambaja, kuwabusu na hata kuwaagiza kucheza densi na mimi. Aghalabu ninapofanya vituko hivyo mtaani na vichochoroni, wenyeji, wageni na watalii hukusanyika kutazama. Baada ya hapo mimi hujipatia fedha,” akasema Bw Abeid.
Kaunti ya Lamu iko na zaidi ya visiwa 35 ambavyo hupatikana kwenye maeneo mbalimbali ya eneo hilo.
Usafiri unaotegemewa kwenye visiwa hivyo ni wa punda, miguu na boti kwani magari hayaruhusiwi kuhudumu kwenye baadhi ya visiwa hivyo, hasa mji wa kale wa Lamu ambao ni wa kihistoria.
Lamu ina zaidi ya punda 10,000, ambapo kisiwa cha Lamu kinaongoza kwa zaidi ya punda 3,000.