Uteuzi wa Kidato cha Kwanza waahirishwa

Uteuzi wa Kidato cha Kwanza waahirishwa

Na DAVID MUCHUNGUH

WANAFUNZI waliofanya Mtihani wa Darasa la Nane (KCPE) mnamo Machi mwaka huu, watalazimika kusubiri zaidi kabla ya kujua shule za upili watakazojiunga nazo.

Matokeo ya uteuzi wa wanafunzi watakaojiunga na shule mbalimbali za sekondari yalifaa kutolewa Ijumaa wiki hii, lakini imeahirishwa kwa wiki mbili hadi Juni 15.

Watahiniwa 1,179,192 waliofanya KCPE wamekuwa wakingoja kwa hamu kujua shule watakazojiunga nazo.

Wakati wa hotuba yake alipokuwa akitangaza matokeo ya KCPE Aprili 15, Waziri wa Elimu Profesa George Magoha alisema kuwa wanafunzi wangejua shule za sekondari watakazojiunga nazo Mei 28. Lakini jana, Prof Magoha hakutoa sababu zozote za kuahirisha shughuli hiyo.

“Wizara ya Elimu inaendelea na mchakato wa kuwapangia wanafunzi shule za sekondari watakazojiunga nazo. Matokeo ya mchakato huo yatatangazwa Juni 15. Nawahakikishia kuwa watahiniwa wote waliofanya mtihani huo watajiunga na shule za upili,” akasema Waziri Magoha.

Kuahirishwa huko kumepokelewa kwa hasira na wazazi wa watahiniwa hao,

“Hatujaridhishwa na hatua hiyo ya Prof Magoha. Tumekuwa tukingojea matokeo ya uteuzi wa wanafunzi ili tujue hatua inayofuatia. Hata wanafunzi waliofanya mtihani watakumbwa na msongo wa mawazo.

“Wanafunzi wanataka kujua shule watakazoenda. Waziri alifaa kutoa sababu kuhusu hatua ya kuahirisha shughuli hiyo,” akasema Bi Catherine Muthoka, mzazi kutoka jijini Nairobi ambaye bintiye anasubiri kujiunga na Kidato cha Kwanza.

Maafisa wa Wizara ya Elimu wako mjini Naivasha ambako wamekuwa wakifanya kazi ya kuhakikisha kuwa watahiniwa wote wanajiunga na shule za sekondari.

Wanafunzi watapangiwa shule kulingana na alama walizopata na shule ambazo wanafunzi walichagua kabla ya kufanya mtihani wa KCPE.

Prof Magoha mwezi uliopita alisema kuwa mfumo unaotumiwa kuwapangia watahiniwa shule ni wa kuaminika na uteuzi huo utakuwa huru na haki.

Wanafunzi wa Kidato cha Kwanza na Darasa la Kwanza wanatarajiwa kuanza masomo yao Julai, kwa mujibu wa kalenda mpya ya masomo.

Kumekuwa na madai kuwa baadhi ya wazazi wamekuwa wakijaribu kutoa hongo kuwezesha watoto wao waliopata alama za chini kujiunga na shule za kitaifa.

You can share this post!

Kampuni za mikate zaonywa dhidi ya kupotosha wateja kuhusu...

Sossion asema mbinu ‘chafu’ za TSC kamwe hazitagawanya...