Wapuuza Uhuru

Wapuuza Uhuru

VITALIS KIMUTAI na BENSON MATHEKA

WANASIASA wamedhihirisha kuwa kamwe hawako tayari kutii amri ya Rais Uhuru Kenyatta aliyepiga marufuku mikutano ya kisiasa na mingineyo kwa lengo la kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona.

Polisi nao wamempuuza Rais Kenyatta kwa kuonyesha ubaguzi katika utekelezaji wa kanuni alizotoa, ambapo wanawaacha wanasiasa kuzivunja, huku wakiwawinda raia wa kawaida kwa visingizio vya kutekeleza sheria hizo.

Wanasiasa na maafisa wakuu serikalini wamepuuza bila kujali masharti ya kupambana na ueneaji wa ugonjwa wa Covid-19, hali inayotoa picha kuwa kanuni hizo zinaendeleza tu ubaguzi dhidi ya raia wa kawaida.

Utekelezaji wa sheria za kukabiliana na virusi vya corona umeanika ubaguzi ambao serikali imekuwa ikiendeleza dhidi ya wananchi.

Naibu Rais William Ruto, waziri mkuu zamani Raila Odinga, aliyekuwa makamu wa rais Kalonzo Musyoka na mwenzake Musalia Mudavadi, ni miongoni mwa wengine ambao wamekuwa wakimwonyesha Rais Kenyatta ‘dharau’ kubwa kwa kuandaa mikutano ya halaiki licha ya kuipiga marufuku.

Cha kutamausha ni kuwa polisi, ambao wanafaa kutekeleza maagizo ya Rais Kenyatta, wamekosa kufanya lolote kuzuia mikutano hiyo inayochochea usambazaji wa Covid-19. Waziri wa Usalama, Dkt Fred Matiang’i na katibu wa wizara ya afya Susan Mochache ambao wanafaa kuwa msitari wa mbele kutekeleza sheria hizo wamekuwa wakizivunja.

Mnamo Septemba 11 wawili hao waliongoza hafla kadhaa kaunti za Nyamira na Kisii walikohudhuria umati wa wakazi.

Polisi pia wamekuwa wakilenga wananchi wa kawaida katika utekelezaji wa kafyu, uvaaji barakoa na kufungwa kwa kilabu za pombe.

Lakini ubaguzi unazuka inapohusisha wananchi wa kawaida, ambapo polisi hutumwa kutekeleza kanuni kwenye hafla za kidini, mazishi, harusi, kufungwa kwa mabaa ifikapo saa moja jioni pamoja na kukamata wasiovaa barakoa na kuwa nje baada ya saa nne za usiku.

Wakati polisi wanapokabiliwa na raia kwa kuwadhulumu wanatumia nguvu. Mnamo Agosti 2 polisi walilaumiwa kwa kuwaua ndugu wawili waliowakamata wa kukiuka kafyu eneo la Kianjakoma, Kaunti ya Embu. Maafisa sita wameshtakiwa kwa mauaji ya kaka hao waliokuwa wanafunzi wa vyuo vikuu.

Wikendi iliyopita katika Kanisa Katoliki la Tegat, kikosi cha polisi kilitumwa kuhakikisha idadi ya waumini haikupita 100 kwenye ibada iliyoongozwa na Askofu (Kanali Mstaafu) Alfred Rotich.

Wiki mbili kabla ya kisa hicho, polisi walifutilia mbali hafla ya kidini katika Kaunti Ndogo ya Bomet kwa visingizio vya kutekeleza sheria za Covid-19.

“Utekelezaji wa sheria za Covid-19 unaonyesha ubaguzi mkubwa. Polisi wanahakikisha wananchi ikiwemo katika maeneo ya ibada hawapiti idadi iliyotangazwa, lakini wanaruhusu mikutano ya wanasiasa inayohudhuriwa na maelfu, wengi wakiwa hawajavaa barakoa,” akasema Rolex Kiprotich Sirmah, mwanasiasa kutoka Bomet Mashariki.

Kwenye mikutano ya wanasiasa pamoja na hafla zingine wanazohudhuria kama vile mazishi na ibada makanisani, polisi wamekuwa wakitazama tu sheria alizotangaza Rais Kenyatta zikivunjwa.

Kulingana na Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Nyeri ya Kanisa Katoliki Antony Muheria, tatizo kubwa katika utekelezaji wa kanuni za kuzuia corona ni wanasiasa.

“Ninaambia wanasiasa wetu wapende nchi yao, waache kuandaa mikutano ya kisiasa ambayo imetambuliwa kama kichocheo kikuu cha maambukizi ya corona,” asema.

Wanasiasa hao wamekuwa wakiandamana na washirika wao maeneo tofauti nchini wanakoandaa mikutano kujipigia debe hata kabla ya msimu wa kampeni za uchaguzi mkuu wa 2022 kutangazwa rasmi.

Bw Odinga ameandaa mikutano kaunti za Kakamega, Kisii, Homa Bay na Mombasa kuvumisha kampeni yake ya Azimio la Umoja mbali na kukutana na makundi kadhaa ambako kanuni za kuzuia corona hazizingatiwi.

kt Ruto amekuwa akipuuza kabisa kanuni hizo akikutana na jumbe kutoka maeneo yote ya nchi katika makazi yake rasmi mtaani Karen, Nairobi, pamoja na kuandaa mikutano ya kisiasa maeneo tofauti.

Mwishoni mwa wiki, Dkt Ruto alizuru maeneo ya Kajiado na Makueni alikohutubia mikutano kadhaa siku moja baada ya kuongoza washirika wake kuendeleza kampeni yake ya hasla kaunti ya Kiambu.

Katika kile kinachodhihirisha kuwa sheria ni za watu wa matabaka ya chini, polisi wamekuwa wakiwanyima Wakenya wakiwemo viongozi wa kidini kibali cha kuongoza hafla zinazokiuka kanuni za wizara ya afya za kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona huku wakiwarusu wanasiasa.

Kuhusu takwimu za maambukizi zilizotangazwa jana, watu 317 walipatikana kuambukizwa na virusi hivyo baada ya watu 6,129 kupimwa, huku wengine 27 wakiaga dunia na kufikisha jumla ya walioangamizwa na ugonjwa huo kuwa 5045.

You can share this post!

‘Wakenya 103 wamefia Uarabuni tangu 2019’

Kaunti zatakiwa kuanzisha mpango tamba wa utoaji chanjo