Na PATRICK KILAVUKA
Mwanasoka chipukizi winga Mbale Mukunda,16, mwanafunzi wa darasa la saba Shule ya Msingi ya Gatina, Kawangware anasema ndoto yake ni kuwa Lionel Messi wa kesho aliyetokea Barcelona kujiunga na PSG.
Yeye ni wa asili ya DRC Congo akiwa kifungua mimba miongoni mwa watoto saba wa familia ya Bw Mukunda Mbilizi na Bi Wakusomba Mukuninwa. Alianza kucheza soka akiwa darasa la pili, Shule ya Msingi ya Mbeleke, DRC Congo kabla familia kuguria nchini na kuendeleza ubabe wa kabumbu anakosomea.
Alipata hifadhi katika timu ya mtaani ya wasiozidi miaka 15 ya Fusion FC kabla jicho pevu la kocha wa Escalators FC Peter Kamau ambayo inashiriki Ligi ya Kaunti, FKF, Nairobi West kuona juhudi zake na kunasa huduma zake.
Isitoshe, alipata fursa ya kushirikishwa katika ya ligi na kupata nafasi ya kusakata michuano sita na kucheka na nyavu mara tatu. Alikuwa miongoni mwa wachezaji walioshiriki katika fainali za mabingwa Ligi ya Kaunti, FKF, Nairobi West uga Ligi Ndogo na kupokea medali baada ya timu yao Escalators kuibuka ya pili bora.
Mwanadimba huyo anasema japo anabanwa na masomo, changamoto imekuwa kusawazisha masomo na talanta! Lakini utaratibu mufti ambao ameuweka kusawazisha mambo unayapatia masomo kipa umbele kisha kutumia wakati wa jioni au ziada kujinoa na kucheza kwenye ligi wikendi.
Chakula ambacho anapenda ni ugali na mboga kwa minajili ya kuupa mwili kinga na nguvu. Angependa kuwa injinia. Mbali na kuazimia kuwa mchezaji wa Manchester City ughaibuini majaliwa. Uraibu wake ni uigizaji na uchoraji.
Fanikio lake ni kwamba, ametambuliwa kuwa winga na jinsi alivyoisadia timu yake ya Escalators katika Ligi kufikia fainali na kupata medali. Wazo la ushauri ni kwamba, kujitahidi, kujinoa na kujituma ni zao la ufanisi.