Habari

Maadhimisho ya Siku ya Valentino yanoga

February 14th, 2018 2 min read

Na WAANDISHI WETU

Kwa Muhtasari:

  • Mwaka huu imeambatana na Jumatano ya majivu, na huenda waliozingatia dini wakakosa kuitilia mkazo
  • Wale wasiokuwa na wa kuandamana ama kusherekehea pamoja siku hii, wanaweza kujipa raha wenyewe!
  • Maeneo yanayovutia watu wengi ni ziwa la Nakuru, makavazi ya Lord Egerton Castle pamoja na hoteli mashuhuri
  • Wakenya wengi wana mpango wa kuwapeleka wapenzi katika hoteli moja mashuhuri

SHAMRASHAMRA za maadhimiso ya Siku ya Valentino inayotambuliwa kuwa ya wapendanao zimeonekana kunoga katika baadhi ya maeneo nchini.

Hata hivyo, siku hii mwaka huu imeambatana na Jumatano ya majivu, na huenda waliozingatia dini wakakosa kuitilia mkazo.

Japo huwafaa wenye kutarajia wapenzi, wake ama waume wao kuwakumbuka, kwa zawadi na njia nyingine, wasiokuwa na wa kuwatunza kwa njia hiyo huenda wakagubikwa na hofu na majonzi.

 

Jipe raha mwenyewe

Hata hivyo, utafiti wa Kisayansi uliotolewa majuzi, unaonyesha kuwa hata wale wasiokuwa na wa kuandamana ama kusherekehea pamoja siku hii, wanaweza kujipa raha wenyewe! Utafiti huo unaeleza kuwa kuna manufaa ya kuwa pekee yako tu.

Unasema kuwa watu hao wana uhusiano thabiti wa kijamii, wako salama kimwili na wanajikuza zaidi wakiwa pekee yao.

Katika kaunti ya Nakuru, sehemu za burudani zimejitayarisha kuwapokea wateja wanaofika kwa maadhimisho ya siku hiyo.

Baadhi ya maeneo yanayotarajiwa kuvutia watu wengi ni ziwa la Nakuru, makavazi ya Lord Egerton Castle pamoja na hoteli mashuhuri.
Makavazi ya ‘Lord Egerton Castle’ yaliyoko eneo la Ngata, Nakuru yana historia pevu katika somo la mapenzi, japo kwa kinaya.

 

Harusi

“Tumekuwa tukipokea wageni wengi haswa wanaofanya harusi, makundi ya vijana wanaokuja kujiburudisha na wapenzi wanaokuja kupunga unyunyu humu. Siku ya Valentino tunatarajia zaidi ya wageni 300,” akasema Emanuel Oduor, mfanyakazi katika makavazi hayo.

“Siku hiyo nina mpango wa kumpeleka mpenzi wangu katika hoteli moja mashuhuri kisha eneo la kujitazamia mazingira mwanana. Nimemnunulia zawadi kemkem,” Kennedy Kimani akaeleza.

Jijini Mombasa, shughuli ziliendelea kunoga huku wauzaji wa maua wakijiweka katika maeneo maalum ambako wanatarajia kupata wateja.

Katika barabara ya Nyerere, tulikutana na Mgeni Juma mwenye umri wa miaka 18 akiuza maua nje ya ukumbi huo.

 

Ripoti za LUCY KILALO, PETER MBURU na KAZUNGU SAMUEL