Shangazi Akujibu

Anataka kunipeleka kwa wazazi ila nimepata habari yeye ‘husoma katiba’ ya mrembo mwingine

July 2nd, 2024 1 min read

Shangazi,

Nimepata habari kuwa mpenzi wangu ana mwanamke mwingine. Nataka tuachane lakini anasisitiza kuwa ananipenda na anataka kunipeleka kwao. Je, atampeleka wapi huyo mwingine?

Mbona wataka kumuacha mpenzi wako kwa kutegemea udaku? Ni vyema kwanza ujue asili na ukweli wa habari hizo. Nia ya mpenzi wako kukupeleka kwao ni thibitisho kwamba anakupenda. Kama unataka kudumisha uhusiano jitenge na umbeya.

Demu jirani yangu amenipagawisha kishenzi

Nimevutiwa kimapenzi na mwanamke jirani yangu katika mtaa ninamoishi. Ninamuona karibu kila siku lakini nimeshindwa kurusha mistari.

Hujasema ni kwa nini umeshindwa kujieleza kwa mwanamke huyo. Usifikiri ni wewe pekee unayemtaka, ukichelewa atanyakuliwa na mtu mwingine. Mwambie ili ujue msimamo wake.

Nilimnasa peupe akila starehe na msupa

Shangazi. Nilimfumania mpenzi wangu na mwanamke mwingine katika maskani ya burudani. Aliniambia ni rafiki yake wanayefanya kazi pamoja. Ajabu ni kwamba mwanamke huyo aliondoka ghafla. Nina wasiwasi.

Hatua ya mwanamke huyo kuondoka ghafla inatia shaka. Inawezekana wana uhusiano wa kisiri na alihofia kwamba iwapo angekaa zaidi ungegundua. Chunguza mienendo yao ujue ukweli kuhusu kinachoendelea kati yao.

Mpenzi sasa anadai rafiki yangu anammezea mate

Mpenzi wangu ni jirani ya rafiki yangu mjini. Ameniambia rafiki huyo anamtaka na amekuwa akienda nyumbani kwake mara kwa mara. Jambo hilo linanitatiza moyoni ingawa bado sijamuuliza rafiki yangu.

Sasa umejua mpenzi wako ni mwaminifu kwako. Ukimuuliza rafiki yako atakana na labda mtakosana. Ili kuepuka ugomvi na kudumisha urafiki wenu, shauriana na mpenzi wako atafute nyumba kwingine mbali na huyo rafiki.