Michezo

Zarika adenguliwa licha ya kupigana kinoma

May 12th, 2024 1 min read

NA CHARLES ONGADI

JUHUDI za bondia Fatuma ‘Iron Fist’ Zarika kunyanyua taji la Madola uzani wa Super Feather ziligonga ukuta aliposhindwa na Kirsty Hill  katika ukumbi wa Winter Gardens, Uingereza, Jumamosi usiku.

Zarika,39, ambaye amekuwa akifanya mazoezi ya kufa na kupona nchini kabla ya kuelekea Uingereza kwa pigano hili, alionyesha mchezo wa hali ya juu akipigana kinyama kuanzia mwanzo hadi mwisho.

Katika pigano hili, Zarika alihakikisha anamweka karibu mpinzani wake na kuwachilia ngumi za kushoto na kulia akielekeza kwa mbavu, tumbo na kichwa zilizomfanya Kirsty kujikunja kila mara kwa uchungu.

Lakini Kirsty aliyekuwa akicheza mbele ya mashabiki wake wa nyumbani, alijibu mipigo ya Zarika kwa ngumi za kushtukiza za kichwa ijapo hazikuonesha madhara yoyote kwa Zarika aliyeonekana na nguvu nyingi.

Baada ya kutamatika kwa pigano hili, idadi wastani ya mashabiki wa Kenya waliohudhuria waliamini bingwa huyu wa zamani wa Dunia wa taji la WBC uzani wa Super Bantam alingelitawazwa mshindi.

Hata hivyo, refa wa pigano hili Kieran McCann alimnyanyua mkono Kirsty baada ya majaji Mark Bates kutoa matokeo ya 94-96 kwa Kirsty, Jamie Kirkpatrick akitoa ushindi wa 97-94 kwa Zarika naye Mark Lyson akitoa ushindi wa 94-96 kwa Kirsty.

Ni matokeo yaliyowaacha mashabiki wa Kenya waliofika ukumbini vinywa wazi huku mashabiki wa Uingereza waliofika kumshangilia bondia wao wakishangilia ushindi wa bondia huyo.

Kirsty,32, aliyeshinda taji hili mnamo Septemba 15, 2023 baada ya kumdengua Vicky Wilkinson katika pigano lililoandaliwa ukumbi wa The Hagar Evens, Uingereza.

Ni ushindi ambao umeimarisha rekodi ya Kirsty akishinda mapigano saba na kushindwa mara mbili na wala hajaandikisha matokeo ya sare.

Kwa Zarika aliyekuwa na matumaini makubwa ya kuleta taji hili nyumbani sasa anasalia na rekodi ya kushinda mapigano 34,18 kwa njia ya KO huku akidenguliwa mara 14 na kupata sare mara mbili.