Habari za Kitaifa

Rex alipigwa risasi mapajani, akavuja damu hadi akakata roho; familia yataka haki itendeke

Na WINNIE ONYANDO June 21st, 2024 1 min read

FAMILIA ya Rex Masai, kijana mwenye umri wa miaka 29 aliyeuawa kwa kupigwa risasi Alhamisi wakati wa maandamano sasa wanataka haki itendeke.

Wakizungumza na Taifa Leo wakiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha, Bi Gillian Munyao, mamake mwathiriwa alisema kuwa mwanawe aliuawa kinyama akitetea haki za wanyonge.

Ndugu na jamaa za Rex Masai, kijana aliyepigwa risasi wakati wa maandamano Alhamisi. Picha|Boniface Bogita

Nasikitika sana mwanangu kuuawa kwa njia kama hiyo. Kama familia, tunaomba haki itendeke.

Bi Munyao alimtaja Rex kama kijana mpole ambaye hapendi vita wala uchochezi.

“Alikuwa ametoka kazini wakati alikutana na kifo chake. Nimempoteza mwanangu kifunguamimba.”

Wanasiasa kama vile Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna ni miongoni mwa watu waliokuja kuifariji familia ya mwathiriwa katika mochari hiyo huku upasuaji wa maiti ukisubiriwa.

Alisema hakuna haja polisi kutumia nguvu kuwatawanya vijana waliokuwa wakiandamana wwa amani.

Familia hiyo bado imepiga kambi katika mochari wakisuburu idhini ya polisi ili mwili wa mwathiriwa ufanyiwe upasuaji.

Kulingana na familia, kijana huyo alipigwa risasi mapajani.