Habari Mseto

Kampuni ya Naboka kusaidia familia za waliopata ajali

May 21st, 2024 1 min read

NA NYABOGA KIAGE

USIMAMIZI wa kampuni ya Naboka Travellers Sacco ambao basi lake lilihusika kwenye ajali katika barabara ya Ushirika na watu tisa kupoteza maisha yao, umesema utasaidia familia zilizoathirika.

Jumanne, walifanya kikao na maafisa wa Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama (NTSA) ili kutoa ripoti ya kina kuhusu ya basi lenye usajili ni KAY 185L. Meneja wa Kampuni hiyo Bw Simeon Makori, alisema kuwa na masikitiko na kutoa rambirambi zao kwa familia husika.

“Muungano wa Naboka Sacco una masikitiko makubwa kwamba basi letu lilipata ajali kwenye barabara na kusababisha vifo vya watu tisa na 15 kujeruhiwa,” alisema Bw Makori. Shughuli za usafiri zilisitishwa kwa kile wasimamizi walisema ni mshikamano na familia zinazoomboleza.

Kiongozi wa Muungano wa Maslahi ya Wenye Matatu Bw Dickson Mbugua alisema wanasubiri kupata uamuzi utakaofanywa na NTSA.

“Tulikuwa na mkutano na wanafunzi na tutakuwa na mwingine. Binafsi nataka kuwashurukuru kwa kufanya maamuzi ya kukosa kuandamana,” alisema Bw Mbugua.