Habari Mseto

Mbunge wa Taveta: Nilipiga ‘ndio’ lakini mkisema hamtaki nitapiga ‘la’ Jumanne


MBUNGE wa Taveta John Bwire ametetea uamuzi wake wa kura ya ‘Ndio’ katika Mswada wa Fedha 2024, akisema kuwa aliunga mkono mswada huo kwa ajili ya maendeleo ya eneo lake. 

Alisema licha ya kupigwa mawe kwa mkondo aliochukua, serikali ina lengo la kujenga barabara mbili kuu za eneo hilo na hivyo kumlazimisha kuunga mkono mswada huo.

Baadhi ya barabara zinazolegwa kujengwa ni ile ya Taveta-Eldoro-Mrabani na ya Cess-Jipe ambazo zitagharimu takriban Sh1.3 bilioni na Sh1.9 bilioni mtawalia.

Aidha alisema kuwa barabara ya Taveta-Illasit iko mpangoni kujengwa kwa Sh8.5 bilioni.

“Kipengele ambacho sikubaliani nacho ni ushuru wa barabara ambao uliongezwa kutoka Sh18 hadi Sh25. Hata hivyo, hizo pesa ndizo zitajenga hizi barabara kwa hivyo nitapingaje?” akasema.

Akiongea katika eneo la Rekeke mjiji Taveta, alisema kuwa wengi wanaopinga mswada huo hawajausoma.

“Nilisoma mswada huo na ile ripoti ya Kamati ya Bunge ya Fedha ndipo nikatoa uamuzi wangu. Yule aliyesoma ripoti hiyo hapa anyoshe mkono juu. Nasikia mnasema kuwa mlinituma nikapinge mswada huo lakini yule ana sababu yake aniambie,” akawaambia wenyeji.

Aidha alisema ushuru huo wa barabara hautaathiri wananchi ambao hawana magari.

“Acheni matajiri kama mimi Bwire tulipe hiyo kodi. Hata hivyo, mkisema hamtaki niunge mkono mswada huo Jumanne nitapiga la,” akasema.