Habari za Kitaifa

Wabunge walazimika kutorokea kwenye afisi zao kupitia kwa kichochoro cha ardhini

Na MWANDISHI WETU June 25th, 2024 1 min read

WABUNGE wamelazimika kukimbia kwa afisi zao zilizoko Bunge Towers kufuatia kuvamiwa kwa Majengo ya Bunge na waandamanaji wanaopinga ushuru kwenye Mswada wa Fedha 2024.

Habari zinazotufikia hivi punde zinasema kwamba pindi tu waandamanaji hao waliojawa na hamaki walipofaulu kuvunja ua wa Bunge kupitia upande wa Uhuru Highway, waliingia na kuvunja vyoo na kufanya uharibifu mkubwa.

Maafisa wa polisi ambao wengi wao walionekana kulemewa na wingi wa waandamanaji hao waliangalia wasijue la kufanya huku vijana wakiingia kila upande mithili ya nyuki.

Awali hali ya mshikeshike ilishuhudiwa karibu na City Hall, wakati polisi walipofyatua risasi zilizoishia kujeruhi watu wanne huku ripoti zingine zikidai kwamba wawili waliaga dunia.