Habari Mseto

Afisa wa KDF alivyomkatakata kasisi aliyemkuta akichovya asali yake


MAAFISA wa polisi katika mji wa Kapsabet, Kaunti ya Nandi wameanzisha uchunguzi kuhusu kisa cha Jumatano usiku ambapo padre wa kanisa ya Kianglikana mwenye umri wa miaka 43, aliyeuawa kinyama na afisa wa KDF kwa tuhuma za uzinifu.

Kulingana na Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Nandi Bw Dickens Njogu, mtu ambaye jina lake halikutambulishwa alifahamisha polisi kwa simu kuhusu kisa hicho mwendo wa saa tatu asubuhi mnamo Alhamisi.

Uchunguzi wa awali ulibaini kuwa Padri James Kemei wa Kanisa la St Barnabas huko Kapsabet, alimtembelea mwanamke huyo ambaye pia wanahudhuria kanisa moja usiku huo bila kujua kwamba mumewe alikuwa amemwekea mtego.

Afisa huyo wa jeshi alifika baadaye na kumkuta Padri akiwa kitandani na mke wake.

“Kwa hasira, afisa huyo alimuua kasisi huyo kwa kumkata sehemu za siri mke wake akitazama. Pia alimsababishia majeraha mabaya kichwani na kumvunja mbavu na miguu. Lilikuwa tukio la kusikitisha sana,” alisema Mark Kiptoo, jirani.

Padri Kemei alikimbizwa katika hospitali ya Kapsabet level 5 akiwa katika hali mahututi na akahamishiwa Hospitali ya Top Hill ya Eldoret ambapo alitangazwa kuwa amefariki alipofika.

Afisa wa KDF ambaye pia alimjeruhi mkewe vibaya aliondoka baada ya kisa hicho.

Mkewe anapokea matibabu katika hospitali moja ya kibinafsi.

Kamanda wa Polisi aliwataka wananchi wa eneo hilo kuacha kuchukua sheria mikononi mwao na kuongeza kuwa iwapo mtu anadhulumiwa anafaa kutoa taarifa kwa polisi badala ya kuzua ghasia.

“Sote tuheshimu utakatifu wa ndoa na kushughulikia mizozo ya ndoa kupitia njia za kisheria,” alisema na kuongeza kuwa mshukiwa amejificha na polisi wanamsaka ili kushtakiwa kwa mauaji.