Serikali yashtakiwa kwa kukosa kufidia walimu, polisi wanaofariki
SERIKALI imeshtakiwa kwa madai ya kukosa kulipa bima ya zaidi ya Sh20 bilioni familia za watumishi wa umma waliofariki au kujeruhiwa kazini, wakiwemo walimu na maafisa wa polisi.
Kesi hiyo iliyowasilishwa katika Mahakama Kuu Nairobi na John Gitonga inadai kuwa serikali imekuwa ikikiuka sheria kwa kushindwa kutoa bima ya lazima na kulipa fidia kwa vifo, ulemavu na majeraha ya kazini kwa mamia ya maelfu ya watumishi wa umma.
Bw Gitonga anasema hali hiyo imeacha familia za marehemu na watumishi waliopata ulemavu bila fidia wanazohakikishiwa na sheria.
Walioshtakiwa ni Wizara ya Fedha, Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), Mamlaka ya Kudhibiti Bima (IRA), Hazina ya Pensheni wa Watumishi wa Umma (PSSF), Tume ya Utumishi wa Umma, Tume ya Kuwaajiri Walimu (TSC), Tume ya Utumishi wa Mahakama (JSC), Tume ya Kitaifa ya Huduma za Polisi, Mwanasheria Mkuu, Bunge la Kitaifa pamoja na kampuni kadhaa za bima.
Kesi hiyo inadai kumekuwa na dosari katika usimamizi wa mipango ya bima ya watumishi wa umma.
Bw Gitonga anakadiria kuwa serikali inadaiwa Sh8.4 bilioni kwa watumishi wa umma, Sh3 bilioni kwa polisi na magereza, na angalau Sh10 bilioni kwa walimu.
Anasema madai hayo yanatokana na usimamizi wa bima za ajali kazini, fidia chini ya Sheria ya Fidia kwa Majeraha Kazini (WIBA), bima ya maisha ya kikundi na bima ya gharama za mazishi.
Anataka mahakama itangaze mpango huo kuwa ni kinyume cha Katiba, iamuru malipo ya madai yote yaliyosalia, ukaguzi ufanywe kwa kina wa fedha na kuagiza mageuzi katika usimamizi wa bima za watumishi wa umma.
Katika hati yake ya kiapo, Bw Gitonga anasema aliamua kwenda mahakamani baada ya dadake aliyekuwa mfanyakazi wa TSC kufariki akiwa kazini huku watoto wake wakikosa kulipwa mafao ya bima licha ya kufuatilia kwa muda mrefu.