Matumizi ya tiba asili na nafasi yake katika afya ya jamii
UNAPOAMKA asubuhi ukiwa na mafua na kukohoa, kuna uwezekano mkubwa kuwa ushauri wa kwanza utapata kutoka kwa mwanafamilia hautakuwa wa kwenda hospitalini.
Utaambiwa, “Chemsha tangawizi, limau kisha ongeza asali.”
Kwa upande mwingine, ukiwa mashambani na unaumwa na tumbo, huenda ukasikia ukiambiwa uchemshe majani au mzizi fulani ambayo wazee wamekuwa wakitumia kwa miaka mingi.
Kwa vizazi vingi, Wakenya wamekuwa wakitegemea mimea, mizizi, mashina ya miti na dawa nyingine za jadi kukabiliana na matatizo mbalimbali ya afya.
Kwa wengine, tiba asili ni sehemu ya maisha ambayo wamerithi kutoka kwa wazazi na mababu zao.
Kwa wengine, ni chaguo la bei nafuu ikilinganishwa na gharama ya matibabu hospitalini.
Lakini kadri magonjwa sugu kama kisukari, saratani na shinikizo la damu yanavyoendelea kuongezeka, matumizi ya dawa za mitishamba yameibua swali muhimu: Je, tiba asili inaweza kuwa sehemu ya suluhu ya matatizo ya afya ya kisasa?
Swali hili lilipewa uzito wakati wa Siku ya Tiba Asili ya Kiafrika, inayoadhimishwa Agosti 31 kila mwaka.
Maadhimisho ya mwaka huu yalijikita katika kutafakari utafiti na maendeleo ya tiba asili kuelekea kufanikisha huduma za afya kwa wote barani Afrika.
Shirika la Afya Duniani (WHO) lilisema siku hiyo inatambua mchango mkubwa wa tiba asili katika kutoa huduma za afya zinazopatikana kwa urahisi, nafuu na zinazokubalika katika jamii nyingi barani Afrika.
Siku hiyo ilitokana na azimio lililopitishwa na mawaziri wa afya wa Afrika mwaka 2000.
Katika jamii nyingi za Kiafrika, maarifa kuhusu mimea inayotumika kama dawa yamepitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.
Mama angejua mmea wa kutumia kumsaidia mtoto aliyekuwa na homa, kikohozi au matatizo ya tumbo, mzee kwa upande mwingine angejua mzizi fulani au shina la mti wa kutibu maradhi fulani.
Tatizo, hata hivyo, ni kwamba sehemu kubwa ya maarifa hayo haikunakiliwa na kuwekwa kwenye kumbukumbu.
Na baadhi yake yanaendelea kupotea kadri wazee wenye maarifa hayo wanavyoaga dunia.
Lakini katika dunia ya leo, wataalamu wanasema maarifa hayo hayawezi kutegemewa kwa historia pekee.
Lazima yapimwe, kufanyiwa utafiti na kuthibitishwa kama dawa hizo ni salama na kama kweli zinafanya kile zinachodaiwa kufanya.
Hii ndiyo sababu mjadala kuhusu tiba asili sasa unahamia kutoka kijijini na sokoni hadi kwenye maabara.
WHO inasema tiba asili inaendelea kuwa sehemu muhimu ya huduma za afya Afrika, lakini kuna haja ya kuimarisha utafiti, ubora wa bidhaa, usalama na udhibiti wake.
Mfano wa juhudi za kuichunguza tiba inayotokana na mimea ni mmea wa ngano unaochipuka, unaojulikana kama wheatgrass.
Mmea huo huvunwa ukiwa mchanga, kabla haujakomaa na kutoa nafaka.
Ingawa unaweza kuonekana kama nyasi za kawaida, wheatgrass imeanza kuvutia watafiti kutokana na virutubisho na kemikali za asili zinazopatikana ndani yake.
Mwanasayansi wa Kenya, Dkt Njoroge Kimani, ambaye ni mtaalamu wa bayokemia ya kimatibabu na sumu, amekuwa akiufanyia mmea huo utafiti kwa zaidi ya miaka 10.
Utafiti wake unalenga kuchunguza usalama wake, thamani yake na nafasi ambayo inaweza kuwa nayo katika kusaidia afya, hasa kwa watu wanaoishi na magonjwa sugu.
Mmea huo unaweza kutumiwa kama juisi, unga au tembe.
Lakini hapa ndipo wananchi wanapaswa kuwa waangalifu.
Kuvutia kwa mmea katika maabara au kuwepo kwa virutubisho ndani yake hakumaanishi moja kwa moja kwamba tayari ni dawa ya kutibu ugonjwa fulani.
Akizungumzia utafiti wake, Dkt Njoroge, alisema lengo lake kuu limekuwa kubaini iwapo mmea huo ni salama na una ufanisi.
“Nimekuwa nikifanya kazi hii ili kubaini ufanisi na usalama wake kwa sababu usalama ni muhimu,” alisema.
Utafiti wake ulianza zaidi ya muongo mmoja uliopita.
Anasema alianza kuchunguza mmea huo mwaka 2014 kupitia tafiti za maabara na nyingine zilizolenga kuchunguza athari zake na usalama wake.
Kilichomvutia zaidi, anasema, ni muundo wa lishe wa mmea huo.
Faida za wheatgrass
Kwa mujibu wake, wheatgrass ina madini na virutubisho kama vile amino acid, nyuzinyuzi za lishe na protini zinazotokana na mimea.
Lakini, anasema, mmea huo si chanzo cha virutubisho pekee. Pia una kemikali zinazojulikana kisayansi kama bioactive compounds, ambazo zinaweza kuwa na athari mbalimbali mwilini.
Dkt Njoroge amekuwa akichunguza hasa kemikali zinazohusishwa na uwezo wa kupambana na mabadiliko yanayoweza kuharibu seli na zile zinazoweza kuathiri mchakato wa uvimbe wa ndani ya mwili.
Anasema watu wengi wanapozungumzia uvimbe, hufikiria jeraha au sehemu iliyovimba na kuonekana kwa macho. Lakini baadhi ya aina za uvimbe hutokea ndani ya mwili.
“Watu wanapozungumzia uvimbe, hufikiria jeraha au kitu kinachoonekana kimevimba. Lakini kuna uvimbe unaotokea ndani ya mwili,” alisema.
Hata hivyo, wataalamu wanasisitiza kuwa matokeo ya tafiti za awali hayapaswi kutafsiriwa kuwa wheatgrass imethibitishwa kutibu magonjwa sugu.
Utafiti wa kina kwa binadamu bado unahitajika kuthibitisha iwapo manufaa yanayoonekana katika maabara yanaweza kutafsiriwa kuwa manufaa halisi kwa wagonjwa.
Kwa sasa, madai kwamba inaweza kuzuia au kutibu magonjwa makubwa yanahitaji utafiti zaidi wa kina kwa binadamu.
Dkt Njoroge anaamini Kenya inahitaji kuwekeza zaidi katika utafiti wa bidhaa za afya zinazoundwa nchini.
Anasema watafiti wanahitaji ufadhili zaidi ili kuendeleza tafiti, kurekodi maarifa ya jadi na kuwapa wananchi habari sahihi kuhusu dawa za asili.
Changamoto moja, anasema, ni kwamba baadhi ya Wakenya huwa na imani zaidi katika bidhaa za afya zinazotoka mataifa ya kigeni huku wakipuuza uvumbuzi unaofanywa nchini.
Kwa mtazamo wake, suluhisho si kupinga dawa za hospitali au matibabu ya kisasa.
Badala yake, bidhaa zinazotengenezwa nchini zinapaswa kufanyiwa uchunguzi wa kisayansi na kutambuliwa pale ushahidi unapothibitisha kuwa ni salama kwa matumizi.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Tiba Asili ya Kiafrika, Waziri wa Afya Aden Duale alisema dawa na mbinu za jadi zinapaswa kufanyiwa utafiti wa kisayansi, kuthibitishwa na kudhibitiwa ipasavyo kabla ya kuunganishwa katika mfumo rasmi wa huduma za afya.
Kwa mujibu wa Duale, serikali iko katika hatua za mwisho za kuandaa mfumo wa sera utakaosaidia kutathmini, kudhibiti na kukuza tiba asili.
Lengo, alisema, ni kuhakikisha kuwa bidhaa zinazotumiwa na wananchi ni salama, zina ubora unaohitajika na zinaungwa mkono na ushahidi wa kisayansi.
“Wajibu wetu ni kuhifadhi kile kilicho na thamani huku tukihakikisha kwamba kila matibabu yanayotolewa katika mfumo wa afya ni salama, yanafaa na yanaungwa mkono na ushahidi,” alisema Duale.
Kauli hiyo inaonekana kugusa kiini cha mjadala kuhusu tiba asili. Kwa upande mmoja, kuna haja ya kuhifadhi maarifa ya jadi ambayo yamepitishwa kwa vizazi.
Kwa upande mwingine, kuna wajibu wa kulinda afya ya wananchi dhidi ya bidhaa ambazo huenda hazijapitia vipimo hitajika.
Duale alisisitiza kuwa tiba asili ya Kiafrika haipaswi kutumika kama mfumo unaoshindana na matibabu ya kisasa.
Badala yake, alisema, mifumo hiyo miwili inaweza kutumika moja kwa moja pale ambapo kuna ushahidi wa kutosha kuhusu usalama na ufanisi wa matibabu.
Kando na hayo, serikali inalenga kuunganisha tiba asili katika mfumo wa huduma za afya nchini ifikapo mwaka 2028.
Mfumo wa sera unaotayarishwa unatarajiwa kuweka njia ya kutathmini na kudhibiti dawa za jadi kabla ya kuingizwa katika huduma rasmi za afya.