Habari

Sifuna na Orengo wazika tofauti zao za kisiasa kuelekea 2027

Na JUSTUS OCHIENG Na RUSHDIE OUDIA September 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

GAVANA wa Siaya, James Orengo na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, wameanza juhudi za kupunguza mvutano uliokuwa ukiongezeka ndani ya vuguvugu la Linda Mwananchi baada ya wiki moja ya ushindani wa kisiasa uliochochewa na tangazo la Orengo kwamba atawania urais.

Viongozi hao wawili walikutana Ijumaa pamoja na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na wasaidizi wao wa karibu katika kikao ambacho duru za ndani zinasema kililenga kuwatuliza wafuasi wao na kuonyesha umoja kabla ya mikutano ijayo ya kisiasa.

Mkutano huo ulifanyika siku chache baada ya Orengo kutangaza hadharani kwamba yuko tayari kushindania tiketi ya urais ya Linda Mwananchi dhidi ya Sifuna au mgombea mwingine yeyote, akisisitiza kuwa umoja wa upinzani haupaswi kuzuia viongozi wenye tofauti za malengo ya kisiasa.

“Hakuna ubaya katika ushindani wa kisiasa ndani ya Linda Mwananchi au upinzani. Muhimu ni kuwa na mchakato wa kuaminika wa uteuzi na hatimaye tutoe mgombea mmoja wa kukabiliana na Rais William Ruto,” alisema Orengo.

Kauli hiyo ilizua wasiwasi miongoni mwa sehemu ya wafuasi wa vuguvugu hilo ambao tayari walikuwa wameanza kujipanga nyuma ya Sifuna kama mgombea wao wa urais.

Baadhi ya viongozi wamekuwa wakimkosoa Orengo kwa kile wanachodai ni kuanzisha ushindani usio katika vuguvugu ambalo kwa kiasi kikubwa lilikuwa limekubaliana kuhusu mgombea wake wa urais.

Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya amesema kaulimbiu ya “Sisi Ndiyo Sifuna” ni ushahidi kuwa wananchi wengi tayari wameamua wanachotaka.

Mbunge wa Bumula Jack Wamboka, ambaye ni mshirika wa karibu wa Sifuna, pia amekuwa mkosoaji mkubwa wa hatua ya Orengo.

“Wakenya tayari wameamua ni nani wanayetaka apeperushe bendera ya vuguguvu hili katika uchaguzi wa 2027,” amesema.

Naye mwanasiasa Pauline Njoroge, akizungumza katika mkutano wa Linda Mwananchi mjini Meru, alisema wafuasi wengi wa Linda Mwananchi wanaamini Sifuna ndiye anafaa kugombea urais.

“Wafuasi wetu wako wazi kabisa kwamba mgombea wao wa urais ni Edwin Sifuna,” alisema.

Hata hivyo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi alisema Linda Mwananchi inamheshimu Orengo kutokana na mchango wake mkubwa katika mageuzi ya kisiasa nchini, huku akisisitiza kuwa vuguguvu hilo lina mifumo ya ndani ya kutatua suala la mgombeaji wa urais.

Kwa mujibu wa vyanzo vilivyoshiriki mazungumzo ya Ijumaa, Sifuna na Orengo walitaka kuonyesha umoja baada ya baadhi ya washirika wao kuanza kushambuliana kupitia majukwaa ya kisiasa.

“Baadhi ya wafuasi wao walikuwa wameanza kueneza mashambulizi hasa dhidi ya Orengo baada ya kutangaza nia ya kuwania urais. Ndiyo maana viongozi hao waliona ni muhimu kukutana na kuonyesha mshikamano,” alisema mmoja wa watu waliofahamu yaliyojiri.

Muda wa mkutano huo unachukuliwa kuwa muhimu huku Linda Mwananchi ikijiandaa kwa mkutano mkubwa wa hadhara mjini Nairobi mnamo Septemba 13.

Inatarajiwa kwamba mkutano huo utatumika kuendeleza ajenda ya vuguvugu hilo na kutangaza hatua zake zijazo za kisiasa.

Duru nyingine zinasema kuwa Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino alihusika pakubwa katika kupanga kikao hicho.

Inadaiwa kuwa Owino, ambaye anahusishwa na azma ya kuwania ugavana wa Nairobi, anataka kuhakikisha Linda Mwananchi inafanya mkutano huo ikiwa imeungana ili kuongeza nafasi zake za kisiasa dhidi ya Gavana Johnson Sakaja.

Akizungumzia mkutano huo, Sifuna alikataa madai kwamba ulifanyika kwa sababu ya mvutano kuhusu urais.

“Hakuna tatizo lolote. Tulikuwa tukipanga mkutano wetu wa Septemba 13,” alisema seneta huyo.

Hata hivyo, wachambuzi wanasema kuingia kwa Orengo katika kinyang’anyiro cha urais kumeweka wazi changamoto kubwa ndani ya vuguvugu hilo.

Wafuasi wa Sifuna wanaamini kuwa tayari amejijengea umaarufu mkubwa kupitia mikutano ya hadhara na shughuli za mashinani. Kwa upande mwingine, Orengo anasisitiza kuwa umaarufu wa mikutano hautoshi kuchagua mgombea wa urais bila mchakato rasmi wa uteuzi.

Orengo amekuwa akinukuu mifano ya historia ya siasa za upinzani nchini, ikiwemo mchakato wa ODM mwaka 2007 na mazungumzo ya upinzani yaliyozaa muungano wa Kibaki-Wamalwa mwaka 2002, akisema kuwa ushindani wa ndani si jambo jipya.