Habari

Mashambulizi mapya ya ujangili yazuka Turkana, Pokot Magharibi

Na SAMMY LUTTA September 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MASHAMBULIZI mapya ya majangili kwenye mpaka wa Turkana-Pokot Magharibi yanatishia mipango ya kurejeshwa kwa biashara ya kuuza petroli katika kituo cha South Lokichar Basin huku viongozi wakionya kuwa operesheni za mafuta hazitaruhusiwa kuendelea pasipo usalama.

Viongozi kutoka Turkana Kusini na Mashariki wameitaka serikali kurejesha usalama, mifugo walioibiwa, kutambulisha na kuwakamata waliohusika na mashambulizi hayo.

Wameonya kuwa watashinikiza oparesheni za petroli kusimamishwa ikiwa hali haitadhibitiwa.

Wanasema visa vya mauaji, mashambulizi na wizi wa mifugo haviwezi kupuuzwa wakirejelea uvamizi wa majuzi katika kijiji cha Lokwar, eneo la Aroo, mapema Septemba 2, 2026, ambapo watu watatu waliuawa, mmoja akajeruhiwa na mifugo kuibiwa.

“Shughuli zote za Gulf Energy katika maeneo yaliyoathirika ni sharti zisimamishwe hadi hali ya kawaida irejee na usalama kuimarishwa.”