Habari

Omar aunga Shahbal kupinga mpango wa kukinga gavana Nassir

Na WINNIE ATIENO September 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIBU Mkuu wa chama cha United Democratic Alliance (UDA), Hassan Omar, ameungana na mfanyabiashara Suleiman Shahbal kupinga juhudi zozote za kisiasa zinazolenga kuwazuia wagombeaji wengine kuwania ugavana kaunti ya Mombasa na kumpa Gavana Abdulswamad Nassir njia rahisi ya kutetea kiti chake mwaka wa 2027.

Omar alisema uamuzi wa nani anapaswa kuongoza Mombasa unapaswa kuachwa mikononi mwa wapigakura na si kufanywa kupitia makubaliano ya viongozi wa kisiasa.

Alisisitiza kuwa kila mwanasiasa anapaswa kurejea kwa wananchi na kujieleza kuhusu rekodi yake ya uongozi badala ya kutegemea mipango ya kutangaza wagombeaji.

“Kusiwe na makubaliano ya kisiasa wala mtu kulazimishwa kujiondoa. Wananchi ndio waamue wanayetaka kuwa kiongozi wao,” alisema Omar.

Kiongozi huyo wa UDA, ambaye pia anawania ugavana Mombasa, alikosoa vikali utawala wa sasa wa kaunti hiyo akidai kuwa umeshindwa kutimiza matarajio ya wakazi.

Alisema wakazi wa Mombasa wana haki ya kuchagua kiongozi mpya na kwamba kiti cha ugavana hakipaswi kuamuliwa kwenye meza za mazungumzo.

Kauli za Omar zinaoana na msimamo wa Shahbal ambaye amekuwa akipinga kile anachodai ni njama ya kisiasa ya kumzuia kuwania ugavana.

Shahbal amesisitiza kuwa atawania kiti hicho licha ya Rais William Ruto kumshauri aendelee kuwekeza katika sekta ya biashara badala ya kuingia tena katika siasa za uchaguzi.

Akizungumza katika hafla ya uwekezaji Ikulu Nairobi hivi majuzi, Rais Ruto alisema mchango mkubwa wa Shahbal kwa taifa ni kupitia uwekezaji unaozalisha ajira na kukuza uchumi.

Hata hivyo, Shahbal alikataa ushauri huo na kutangaza kuwa jina lake litakuwa kwenye kura mwaka wa 2027.

Mfanyabiashara huyo pia alidai kuwa baadhi ya viongozi wa kisiasa wanatumia miundo ya vyama na hoja ya kutengewa maeneo ya kisiasa ili kuamua nani anapaswa kugombea viti mbalimbali vya uongozi.

Wakati huo huo, baadhi ya madiwani kaunti ya Mombasa wamemtetea Gavana Nassir na kumtaka Shahbal kutii ushauri wa Rais.

Wamesisitiza kuwa gavana huyo ana rekodi nzuri katika sekta za afya, elimu na maendeleo mengine ya kijamii.

Mvutano huo umeweka Omar na Shahbal katika muungano usio wa kawaida.

Ingawa wote wawili wanapania kugombea ugavana wa Mombasa na huenda wakawa wapinzani wakubwa baadaye, kwa sasa wanashirikiana kupinga juhudi zozote za kumhakikishia Nassir muhula wa pili kupitia makubaliano ya kisiasa.

Huku Shahbal akisisitiza kuwa hatajiondoa kwenye kinyang’anyiro, Omar akiendelea kufanya kampeni zake na Nassir akitetea utawala wake, ushindani wa ugavana Mombasa unaonekana kuwa miongoni mwa vita vya kisiasa vitakavyovutia macho ya wengi kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.