Akili Unde ilivyotumiwa kupiga jeki Wandayi na kuumbua upinzani
KAMPUNI ya teknolojia kutoka Amerika imefichua operesheni ya kisiasa Kenya iliyotumia Akili Unde (AI) kueneza ujumbe wa kisiasa kwa njia iliyolenga kuonekana kana kwamba unatoka kwa wananchi wa kawaida.
Kampuni ya Anthropic, inayomiliki mfumo wa AI wa Claude, ilisema iligundua akaunti iliyokuwa ikitumiwa na mtu mmoja kuzalisha kwa wingi maudhui ya kisiasa.
Ujumbe huo uliundwa ili kuonekana kama maoni ya kawaida ya wananchi huku ukimsifu Waziri wa Kawi na Petroli Opiyo Wandayi na wakati huo huo kueneza madai kwamba, upinzani ulikuwa ukisambaratika kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, sehemu kubwa ya maudhui hayo ilimsifu Wandayi kwa madai ya kusaidia kusitisha ongezeko la ushuru wa umeme wa Kenya Power. Ujumbe huo ulitumia lebo za mitandaoni kama #PowerReliefKE na #PoweringTheNewKenya ili kuongeza usambazaji wake na kuonekana kama unaungwa mkono na wananchi wengi.
Anthropic ilisema operesheni hiyo ilikuwa imepangwa kwa ustadi mkubwa, huku AI ikitumika kuzalisha makundi ya ujumbe 50 kwa wakati mmoja uliokuwa tayari kuchapishwa kwenye majukwaa mbalimbali ya mitandao ya kijamii.
Mbali na kumsifu Wandayi, mtandao huo pia ulisambaza madai kuwa muungano wa upinzani ulikuwa ukikumbwa na migawanyiko.
Ripoti hiyo ililenga moja kwa moja aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na Rais (mstaafu) Uhuru Kenyatta kwa kuendeleza simulizi za migawanyiko ndani ya upinzani.
Hata hivyo, Anthropic ilisema kampeni hiyo haikufanikiwa kuwashawishi wananchi halisi. Kampuni hiyo iliorodhesha operesheni hiyo katika kiwango cha chini kabisa cha ushawishi, ikisema shughuli zake zilibaki miongoni mwa akaunti bandia na kushawishi wachache mtandaoni.
Ripoti hiyo imeibua hofu kuhusu matumizi ya AI katika siasa za Kenya kuelekea uchaguzi wa 2027. Wataalamu wanaonya teknolojia hiyo inaweza kutumiwa kutengeneza hisia za umma zisizo za kweli kwa kuzalisha maelfu ya jumbe zinazoonekana kutoka kwa raia wa kawaida.