Waboni wataka fidia kwa ‘kuharibiwa maisha’ na operesheni ya KDF
JAMII ya Waboni katika Kaunti ya Lamu inaishinikiza serikali ya kitaifa kuwalipa fidia kwa kutatiza hali yao ya kawaida ya kimaisha kwa miaka 11 ambayo oparesheni ya kupambana na ugaidi imekuwa ikiendelezwa eneo hilo.
Kulingana nao, oparesheni ya kukabiliana na magaidi wa Al-Shabaab katika Msitu wa Boni iliyoanza mwaka wa 2015, imewazuia kuishi walivyozoea kwa kuwinda wanyamapori, kuchuma matunda ya mwituni na kuvuna asali asili msituni.
Wakiongozwa na Diwani wa Zamani wa Basuba, Bw Mohamed Delo, waliitaka serikali ya kitaifa kuwalipa fidia ili wagharamie shughuli nyingine za kimaisha zisizowahitaji kuingia msituni.
“Ingekuwa haki kama walivyolipa wavuvi walioathiriwa na Bandari ya Lamu Sh1.76 bilioni basi pia na sisi tufidiwe sawia,” akasema Bw Delo, akisisitiza kuwa ombi lao halimaanishi wanapiga vita serikali.
Bw Omar Bwana Barissa, mzee wa kijiji cha Basuba, alisema jamii hiyo pia ina madhabahu ya kitamaduni ndani ya msitu wa Boni.
“Tangu operesheni ianzishwe hata kufika huko ndani ya msitu angalau kuomba haiwezekani,” akasema Bw Barissa.
Bi Halima Musa, mkazi wa kijiji cha Mararani, alisema wamejaribu kubadili maisha kwa kuingilia kilimo, lakini wanakumbwa na changamoto ya uvamizi wa wanyamapori wanaoharibu mashamba yao kila mara.
Kamishna wa Kaunti ya Lamu, Bw Stephen Sangolo alisema bado hajapokea malalamishi rasmi kutoka kwa jamii hiyo kuhusu fidia.