Wataalamu waeleza kwa nini kuna baridi kali Nairobi mwezi huu wa Agosti
KWA Wakenya wengi, Agosti umekuwa mwezi wa kuvaa nguo nzito, kujifunika blanketi na baridi kali isiyo ya kawaida asubuhi.
Nairobi na maeneo ya nyanda za juu katikati mwa nchi yamekuwa yakishuhudia hali hiyo hadi mchana, jambo linalowafanya wengi kujiuliza ni kwa nini ilhali msimu wa kiangazi unakaribia kufika mwisho.
Lakini wataalamu wa masuala ya hali ya hewa wanasema baridi ya Agosti si jambo lisilo la kawaida bali ni sehemu ya mfumo wa kawaida wa msimu unaochangiwa na mabadiliko ya tabianchi katika sehemu ya Kusini mwa Dunia.
Mtaalamu wa Hali ya Hewa katika Mamlaka ya Huduma za Hali ya Hewa Kenya (KMSA), Christine Maswi, alisema Agosti ni miongoni mwa miezi yenye baridi zaidi nchini.
“Kwa kawaida, Agosti huhesabiwa kuwa mwezi wa baridi kwa sababu uko katika msimu wa baridi nchini, wakati upepo kutoka kusini-mashariki huleta hewa baridi na yenye unyevunyevu kutoka Bahari Hindi,” alisema.
Kulingana naye, hali ya hewa ya muda mrefu huchunguzwa kwa kutumia takwimu zilizokusanywa kwa angalau miaka 30 ili kubaini hali inayochukuliwa kuwa ya kawaida katika eneo fulani na msimu fulani.
Chanzo cha baridi hiyo kinaanzia maelfu ya kilomita kusini mwa Kenya, ambako kwa sasa ni majira ya baridi.
Joto linaposhuka katika sehemu hiyo, mifumo huimarika. Mifumo hiyo huathiri upepo kuelekea kaskazini na kuleta hewa baridi Afrika Mashariki.
Mifumo miwili muhimu ni St Helena High, iliyoko upande wa kusini-magharibi mwa bara la Afrika katika Bahari ya Atlantic na Mascarene High, iliyoko upande wa kusini-mashariki wa bara hilo, karibu na Madagascar.
Mifumo hiyo huwa muhimu zaidi wakati wa majira ya baridi katika sehemu ya Kusini ma Dunia.
Kwa hivyo, mifumo hiyo inapokuwa na nguvu, husaidia kusukuma hewa baridi kuelekea Kenya.
“Kadiri mifumo hii inavyoimarika, husukuma hewa baridi kutoka kusini. Ndiyo maana Nairobi, nyanda za juu katikati mwa nchi na sehemu za mashariki mwa Kenya zinaweza kuwa na baridi kali hasa Juni, Julai na Agosti,” Bi Maswi alisema.
Maeneo yanayoathirika ni pamoja na Machakos, Makueni, Kitui na Taita Taveta, ambako wakazi hupata asubuhi zenye baridi na wakati mwingine hali hiyo huendelea kwa siku nzima.
Mchakato huo pia unahusishwa na mahali ilipo Ikweta. Hewa yenye joto karibu na Ikweta hupanda, na hivyo kutoa nafasi kwa hewa baridi kutoka kusini kuingia.
Hata hivyo, nguvu za mifumo hiyo hubadilika kutoka siku moja hadi nyingine. Hilo ndilo linalofanya hali ya hewa ya Agosti kuwa isiyotabirika wakati mwingine.
“Siku moja inaweza kuanza kwa baridi kali kabla joto mchana, huku siku inayofuata ikiwa na mawingu na baridi siku nzima,” alisema.
Utabiri wa KMSA wa Juni, Julai na Agosti ulionyesha kuwa maeneo ya nyanda za juu mashariki mwa Bonde la Ufa, yakiwemo Nairobi na sehemu za nyanda za chini kusini-mashariki, yangeshuhudia hali ya baridi na mawingu hadi nusu ya kwanza ya Septemba.
Hata hivyo, utabiri mpana wa nchi ulionyesha uwezekano wa joto kuwa juu ya wastani.