Habari

Ndindi Nyoro akoroga hesabu za Gachagua Mlimani

August 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KIONGOZI wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua anakabiliwa na changamoto mpya katika juhudi zake za kudhibiti siasa za eneo la Mlima Kenya, mwezi mmoja tu baada ya ushindi mkubwa wa chama chake katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.

Katika uchaguzi huo wa Julai 17, mgombeaji wa DCP, Kamau Ngotho alipata kura 35,440, sawa na asilimia 85 ya kura zote, dhidi ya mgombeaji wa United Democratic Alliance (UDA) aliyeungwa mkono na Rais William Ruto, Muchina Nyaga, aliyepata kura 5,450.

Ushindi huo ulimpa Bw Gachagua nguvu mpya na kumfanya kujitangaza kuwa kiongozi asiye na mpinzani wa kisiasa katika Mlima Kenya, huku akitaja DCP kama chama chaguo la wakazi wa eneo hilo.

Katika uchaguzi huo, Jubilee ya Rais mstaafu Uhuru Kenyatta ilipata kura 198 huku Party of National Unity (PNU) ya aliyekuwa Gavana wa Meru Peter Munya ikipata kura 28.

Lakini mwezi mmoja baadaye, Bw Gachagua anakabiliwa na upinzani mpya, huku hatua ya Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro kujiunga na People’s Party of Kenya (PPK) na kuwa kiongozi wake ikiwa changamoto kubwa zaidi.

Bw Nyoro anasema chama chake ni sehemu ya upinzani na kinalenga kushirikiana na vyama vingine kupata mgombea mmoja wa urais kwa uchaguzi mkuu wa mwaka ujao, pamoja na kuondoa serikali ya Rais Ruto madarakani.

Hata hivyo, Bw Gachagua na washirika wake wamemtaja Bw Nyoro kama mpinzani anayelenga kuvuruga juhudi za kuunganisha kura za Mlima Kenya.

“Mlima ni mmoja, chama ni kimoja (DCP), na kiongozi wa eneo ni mmoja (Gachagua),” alisema Kaimu Katibu Mkuu wa DCP John Methu, ambaye pia ni Seneta wa Nyandarua.

Bw Nyoro, hata hivyo, amesisitiza kuwa yeye ni kiongozi halisi wa upinzani anayelenga kuimarisha ajenda ya upinzani.

“Nitafanya kazi na viongozi wote wa upinzani, akiwemo Bw Gachagua, na chama changu hakitakuwa mahali pa kukimbilia watu waliokataliwa na Mlima ambao wamekuwa wakitukana DCP na uongozi wake,” alisema.

“Najua kuna wanaonitilia shaka. Lakini baada ya muda mtaona msimamo wangu kamili katika kupinga na kuondoa serikali hii madarakani.”

Mchanganuzi wa siasa Gasper Odhiambo alisema Bw Nyoro ana haki ya kidemokrasia kuanzisha chama na kujiunga na upinzani, lakini muda na namna alivyoingia kwenye siasa za upinzani huenda zikamfanya akabiliane na upinzani mkali.

“Bw Gachagua ana haki yote kumchukulia Bw Nyoro kuwa mpinzani wake. Swali ni kwa nini Bw Nyoro alisubiri hadi Bw Gachagua aondolewe kwa kura ya kutokuwa na imani, akabiliane na makundi ya wahuni na maafisa wa polisi waliopotoka, ndipo aanze kuhamasisha Mlima Kenya kuingia upinzani,” alisema.

Bw Odhiambo alisema Bw Gachagua mwenyewe alipitia upinzani kama huo baada ya kuondolewa kwenye wadhifa wa Naibu Rais.

Alisema wakati huo Jubilee na PNU tayari vilikuwa katika upinzani.

“Bw Nyoro ameingia kushindana na Bw Gachagua na DCP. Kisichojulikana ni kama anafanya hivyo kwa niaba yake mwenyewe au kuna nguvu iliyojificha nyuma ya pazia la siasa.”

Bw Odhiambo pia alikumbusha kuwa kabla ya Bw Gachagua kuondolewa madarakani Oktoba 2024, washirika wa Bw Nyoro katika Kaunti ya Murang’a, wakati huo wakiongozwa na Seneta Joe Nyutu, walikuwa wamemuonya Rais Ruto kuwa angehatarisha kiti chake ikiwa angemwacha Bw Gachagua na kumchagua Bw Nyoro.

“Upinzani wa Bw Nyoro dhidi ya Bw Gachagua si jambo jipya. Umekuwepo tangu 2022,” alisema.

Alisema katika shughuli zote rasmi za Bw Gachagua katika Mlima Kenya akiwa Naibu Rais, Bw Nyoro hakuhudhuria hata moja.

“Wakati Bw Gachagua aliondolewa mamlakani na kujitahidi kujijenga kisiasa upya, Bw Nyoro alikuwa amekaa katikati. Sasa kwa kuwa Bw Gachagua anaonekana kurejea kwa nguvu, Bw Nyoro anaingia katika uwanja huo akiwa na chama na azma ya kushindana naye. Bw Nyoro ana mengi ya kueleza,” alisema.

Katika mkutano wa kisiasa Kiharu Agosti 19, Bw Nyoro aliwaomba wakazi wamuamini na akasisitiza kuwa yeye si msaliti.

“Ni kwamba mamlaka huchukuliwa, hayapeanwi. Lazima nijionyeshe kwa njia bora itakayonisaidia kutimiza malengo yangu,” alisema.

Alisema atawasimamisha wagombeaji katika uchaguzi wa 2027 na pia atamenyania nafasi ya kuwa mgombea urais wa upinzani.

“Nina nia njema na nawaomba sote tuvumiliane,” alisema.

Kuingia kwa Bw Nyoro katika uwanja huo kunatokea wakati Naibu Rais Kithure Kindiki anaonekana kuunga mkono juhudi za kuunda mrengo tofauti wa kisiasa Mlima Kenya Mashariki.

Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku ameibuka kama mmoja wa watetezi wakuu wa mpango huo.

Bw Ruku anataka Meru, Tharaka Nithi na Embu kuungana chini ya Prof Kindiki na kisha kujadiliana na Rais Ruto kuhusu nafasi yao katika serikali ijayo.

Ingawa Prof Kindiki amekuwa akisema hadharani kuwa Mlima Kenya unapaswa kuwa kitu kimoja, wazee kutoka Meru na Embu tayari wamemtangaza kuwa msemaji wao.

Katika ishara nyingine ya mgawanyiko huo, Prof Kindiki alisema aliyekuwa Gavana wa Meru Kiraitu Murungi amepewa jukumu la kushirikiana na Rais mstaafu Kenyatta kuhakikisha kuna ushirikiano unaolenga “kuwazuia wapiga kura wa Mlima Kenya kuchagua upinzani mwaka 2027”.

Wakati huohuo, Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri na mwenzake wa Ndia George Kariuki wameanzisha mikakati ya kisiasa inayolenga kupunguza ushawishi wa Bw Gachagua.

Bw Kiunjuri anaripotiwa kuratibu vyama vidogo vinavyomuunga mkono Rais Ruto katika eneo la Mlima Kenya, huku Bw Kariuki akijenga mtandao wa viongozi wa mashinani wanaounga mkono msimamo wake.