El Nino: Shirika latoa tahadhari kwa serikali za Afrika Mashariki
Serikali za Afrika Mashariki zimehimizwa kuwekeza mapema katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi badala ya kusubiri mafuriko na ukame kutokea ndipo zianze kutoa fedha za dharura.
Shirika la Vi Agroforestry limesema maandalizi hayo ni muhimu huku utabiri ukionyesha uwezekano wa mvua nyingi na mafuriko katika maeneo ya Afrika Mashariki kati ya Oktoba na Desemba mwaka huu.
Shirika hilo limesema El Niño haifai kuonekana kama tishio la msimu mmoja pekee, bali ni ishara ya haja ya kuimarisha uwezo wa jamii kukabiliana na majanga ya hali ya hewa.
Kwa mujibu wa shirika hilo, uharibifu wa ardhi, maeneo ya vyanzo vya maji na maisha ya wakulima umeongeza madhara yanayosababishwa na mvua kubwa, mafuriko na ukame.
Utabiri wa hivi karibuni unaonyesha kuwa baadhi ya maeneo ya Afrika Mashariki yanaweza kupokea mvua nyingi kuliko kawaida katika msimu wa Oktoba hadi Desemba, jambo linaloweza kusababisha mafuriko, maporomoko ya ardhi, uharibifu wa mazao na kuhama kwa familia.
Vi Agroforestry imesema serikali zinapaswa kuelekeza fedha zaidi kwa wakulima wadogo, wanawake, vijana na wafugaji ambao wako mstari wa mbele katika kusimamia ardhi na maji.
Shirika hilo limependekeza kupanuliwa kwa kilimo-misitu, ambapo miti hupandwa pamoja na mazao na mifugo, kama njia mojawapo ya kupunguza madhara ya mabadiliko ya tabianchi.
Limesema miti na udongo wenye afya husaidia kupunguza kasi ya maji yanayotiririka, kuzuia mmomonyoko wa udongo na kuongeza uwezo wa ardhi kuhifadhi maji.
Kwa wakulima, miti pia inaweza kuwa chanzo cha matunda, chakula cha mifugo, kuni na kipato wakati mazao yanapoharibiwa na hali mbaya ya hewa.
Vi Agroforestry pia imetaka serikali kuwekeza katika uvunaji wa maji, uhifadhi wa udongo, urejeshaji wa maeneo ya mito na vyanzo vya maji, vitalu vya miti na mifumo ya kilimo inayostahimili mabadiliko ya hali ya hewa.
Shirika hilo limesema mifumo ya kutoa tahadhari mapema inapaswa kuimarishwa ili wakulima wapate taarifa kwa wakati na kuchukua hatua kabla ya mvua kubwa kuanza.
Aidha, limewataka wafadhili, taasisi za kifedha na kampuni binafsi kuongeza fedha kwa miradi inayoongozwa na jamii.
Limesema wanawake, vijana, wakulima wadogo na wafugaji hawapaswi kuonekana kama wapokeaji wa msaada pekee, bali washirikishwe katika kupanga na kutekeleza miradi ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Vi Agroforestry imesema ingawa maandalizi ya dharura kama kusafisha mitaro na kuimarisha huduma za uokoaji ni muhimu, hatua hizo hazitoshi bila uwekezaji wa muda mrefu.
“El Niño itapita, lakini hali ya hewa isiyotabirika itaendelea,” shirika hilo limesema.
Limesema hatua zinazochukuliwa sasa ndizo zitakazoamua iwapo majanga yajayo yataendelea kusababisha hasara kubwa au jamii zitakuwa na uwezo wa kukabiliana nayo.