Akili MaliMakala

Kiwango cha njaa duniani chapungua huku ukame ukitishia mavuno nchini Kenya

Na SAMMY WAWERU August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KIWANGO cha njaa duniani kimepungua kwa mwaka wa tatu mfululizo, lakini dunia bado i mbali kuwahi lengo la kutokomeza njaa ifikapo 2030, ripoti mpya ya Umoja wa Mataifa (UN) imefichua.

Makala ya 2026 ya ripoti ya Hali ya Usalama wa Chakula na Lishe Duniani, kwa Kiingereza ‘the State of Food Security and Nutrition in the World (SOFI) inaonyesha kuwa idadi ya watu wanaokabiliwa na njaa ilipungua kutoka asilimia 8.6 mwaka 2022 hadi asilimia 7.8 mwaka jana, 2025, punguo hilo likiwa sawa na karibu watu milioni 645 duniani.

Hata hivyo, mafanikio hayo bado yako hatarini kutokana na mabadiliko ya tabianchi, kupanda kwa bei ya chakula, migogoro katika nchi zinazounda malighafi ya mbolea na ukosefu wa usawa kiuchumi.

Akizindua ripoti hiyo mwezi uliopita, Julai, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO), Dkt Qu Dongyu, alionya kuwa athari za tabianchi zinaweza kurejesha nyuma mafanikio yaliyopatikana na kusababisha mamilioni ya watu kukabiliwa na ukosefu wa chakula.

“Athari za mabadiliko ya tabianchi zisipodhibitiwa, zaidi ya watu milioni 500 duniani wanaweza kuwa katika hatari ya kukumbwa na njaa,” alisema Dkt Qu.

Aidha, alizitaka nchi kuongeza uwekezaji katika mifumo ya chakula inayostahimili tabianchi, kuimarisha uzalishaji, kuboresha mitandao ya usambazaji na kufanya chakula kupatikana kwa bei nafuu.

Ripoti hiyo ilitolewa kwa pamoja na FAO na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa, yakiwemo IFAD, WFP, WHO na UNICEF.

Ukame unaendelea kushuhudiwa katika baadhi ya kaunti nchini. Picha|Sammy Waweru

Dkt Qu alisema ingawa kiwango cha njaa duniani kimepungua, Afrika bado inakabiliwa na baa la njaa. Ripoti inaonyesha kuwa watu milioni 309 barani Afrika wanakabiliwa na njaa, sawa na mtu mmoja kati ya kila Waafrika watano. Aidha, asilimia 66.6 ya Waafrika hawawezi kumudu lishe bora.

Huku dunia ikiandikisha kupungua kwa njaa, Kenya inakabiliwa na tishio la uhaba wa chakula kutokana na taarifa za kukauka kwa mazao katika maeneo muhimu ya uzalishaji, hasa Bonde la Ufa. Wakulima wameelezea wasiwasi kuhusu mahindi kukaukia mashambani kutokana na kuchelewa kwa mvua na vipindi virefu vya ukame.

Hali hiyo inatarajiwa kuwa mbaya zaidi kufuatia El Niño inayopaniwa kushuhudiwa Oktoba 2026, wakulima wakihofia mimea na mazao kidogo yaliyosalia shambani kusombwa na mafuriko.

Athari za mabadiliko ya tabianchi haswa kiangazi na ukame zinatishia mavuno, usalama wa chakula na mapato ya wakulima wadogo wanaotegemea kilimo cha kutegemea mvua.

Data kutoka AGRA pia inaonyesha kuwa shinikizo la tabianchi ni tishio kubwa kwa uzalishaji wa chakula barani Afrika.

Mvua ya El Niño inayotarajiwa kuendelea hadi mwishoni mwa 2026 na mwanzoni mwa 2027, kilele chake wataalamu wa hali ya hewa wanaonya kitakuwa joto kali na ukame Afrika Mashariki na Kusini.

FAO imezitaka nchi kuharakisha ukumbatiaji wa matumizi ya teknolojia zinazostahimili mabadiliko ya tabianchi, kuboresha mifumo ya upatikanaji wa fedha, mbegu bora na mifumo ya umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa kutumia mifereji (irrigation). “Ni muhimu serikali za nchi za Afrika zijiandae vilivyo ili kukabiliana na tabianchi,” akahimiza Dkt Qu.

Wataalamu wanahimiza wakulima kukumbatia teknolojia za kisasa kuzalisha chakula. Pichani, kabichi zilizokuzwa Isiolo ambayo ni kaunti kame. Picha|Sammy Waweru

Ripoti ya UN pia inaonyesha kuwa watu bilioni 2.7 hawakuweza kumudu lishe bora mwaka 2025, ingawa idadi hiyo ilipungua kutoka bilioni 3 mwaka 2021.

Gharama ya lishe bora duniani imefikia dola za PPP 4.28 kwa mtu kwa siku, huku Afrika ikiwa dola 4.33. Bei ya juu ya matunda, mboga na vyakula vingine vyenye virutubisho inaendelea kuzuia familia nyingi kumudu mlo bora na kamilifu.

Abdurakhmonov Ibrokhim Yulchievich, Waziri wa Kilimo wa Uzbekistan, akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti hiyo alisema mageuzi katika kilimo yanahitaji matumizi ya teknolojia za kisasa na mifumo mipya ya ufadhili.

“Teknolojia za akili bandia, ndiyo Artificial Intelligence (AI) zinaweza kusaidia kuunda hifadhi ya data za wakulima, kurahisisha upatikanaji wa mikopo na kupunguza hatari kwa taasisi za kifedha,” akasema Waziri Ibrokhim.

FAO imesisitiza kuwa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi unahitajika, huku uwekezaji zaidi ukipaswa kuelekezwa katika teknolojia zinazolinda uzalishaji wa chakula na kusaidia wakulima kustahimili athari za tabianchi.