• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 6:27 PM
Chuo cha kiufundi chajengwa mjini Ruiru

Chuo cha kiufundi chajengwa mjini Ruiru

NA LAWRENCE ONGARO

WANAFUNZI wanaokamilisha Kidato cha Nne watanufaika wakijiunga na chuo cha mafunzo ya anuwai kinachofahamika kama Vocational Training College Centre Gatong’ora katika kaunti ndogo ya Ruiru.

Chuo hicho kitagharimu Sh57 milioni kutokana na mipango ya serikali kupitia ushirikiano wa Hazina ya Ustawi wa Maeneobunge (NG-CDF) kwenye ardhi ya ukubwa wa ekari saba.

Akizungumza katika kituo hicho mnamo Alhamisi alipozuru kujionea ujenzi wake, mbunge wa Ruiru, Simon King’ara alisema tayari wanafunzi wapatao 100 wa muhula wa kwanza wamejisajili wakisubiri kujiunga na chuo hicho kitakapokamilika hivi karibuni.

Mbunge wa Ruiru, Simon King’ara akihutubu. PICHA | LAWRENCE ONGARO

Alisema chuo hicho kitaendeshwa na chuo cha kiufundi cha Kabete National Polytechnic.

Mbunge huyo aliwarai wanafunzi wanaokamilisha shule kujisajili ili kupata ujuzi wa kiufundi.

Baadhi ya kozi zitakazoendeshwa katika chuo hicho ni uchomeleaji wa vyuma, umekanika, umeme, kurekebisha mabomba ya mifereji,  na maswala ya teknolojia.

“Ninawarai wanafunzi wote waliokamilisha shule wajitume na chuo hicho ili waweze kupata ujuzi wa kujiendeleza kimaisha,” alieleza Bw King’ara.

Mbunge huyo alipongeza rais William Ruto kwa kufadhili chuo hicho na vifaa vya dhamani ya Sh 100 milioni ambapo utanufaisha wakazi wa Ruiru katika siku zijazo.

Mbunge huyo aliandamana na naibu kamishna wa Ruiru Bi Margaret Mbugua, ambaye alitoa hakikisho kuwa walanguzi wa dawa za kulevya watakabiliwa vilivyo kwa kuchukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria.

“Serikali iko chonjo kuwanyaka wahalifu wanaosumbua wananchi eneo la Ruiru,” alisema Bi Mbugua.

Rasi yaani principal wa chuo cha Kabete National Polytechnic Okumu Odhiambo alitoa wito kwa vijana wengi wawe mstari wa mbele kujiunga na chuo cha kiufundi cha Gatong’ora mjini Ruiru.
  • Tags

You can share this post!

Gareth Bale aangika daluga zake katika ulingo wa soka akiwa...

Kioni atabiri Kenya Kwanza itakufa 2027

T L