NA PATRICK KILAVUKA
MATHEW Joshua, 15, alivutiwa na jinsi ala ya muziki wa kiasili Urutu (zeze) ilivyokuwa ikichezwa kwa namna ya kuifanya ‘kuongea’ ili kuwasilisha ujumbe maalum.
Hivyo basi, akachochewa zaidi kujua mbichi na mbivu kuhusu stadi zinazotumiwa na mchezaji kukifanya chombo hiki ‘kuwasiliana’ na binadamu mwenye ujumbe wa kufikisha kwa jamii.
Kwa mujibu wa Joshua, ala hii hutumiwa kutoa sauti ambayo ikisikilizwa kwa makini, huwa inapitisha mawasiliano kuhusu suala fulani muhimu.
Joshua ni mwanafunzi wa darasa la nane katika shule ya msingi ya Kibera, kaunti ndogo ya Kibra, Kaunti ya Nairobi.
Alianza kucheza isukuti akiwa mwanafunzi wa darasa la kwanza katika shule ya msingi ya Laini Saba, Kibera, kabla kuwa na kiu ya kucheza chombo hiki mwaka huu kwa maandalizi ya mashindano ya tamasha za muziki na drama miongoni mwa shule za msingi.
“Nilipata mshawasha wa kucheza isukuti kutoka kwa mchezaji Harez Odhiambo na ndugu yangu Tonny Foltrigg ambao walikuwa wakicheza kwa umahiri kabla kugeukia urutu,” anasema Joshua.
Alivutiwa sana na mkufunzi wake wa zeze, Samuel Jangoma, ambaye alikuwa akicheza chombo hicho kwa weledi na ustadi mkubwa alipokutana naye kwa mara ya kwanza.
Hata hivyo, alipokuja shuleni mwao kwa minajili ya kuwaanda kwa mashindano ya tamasha za drama, mwalimu wao wa drama, Ramadhan Maimuna, aliyekuwa amekitambua kipawa chake, alimhimiza kujua zaidi baada ya kumtia katika mkondo wa mkufunzi Jangoma ambaye alianza kumnoa kwa muda wa wiki moja.
Joshua ameweza kukichezea kikundi cha drama shuleni mwao na wakafuzu hadi kiwango cha Kanda ya Nairobi katika mashindano yaliyofanyika katika shule msingi ya St Georges, Nairobi. Waliibuka wa kwanza katika kiwango cha kaunti ndogo ya Kibra kwenye mashindano hayo.
Joshua ni wa pili kuzaliwa katika familia ya watoto sita wa Bw David Ayuko na Bi Millicent Awino. Anasema zeze ni ala ambayo anafurahia sana kuicheza kwani inampa mtu msisimko wa ndani unaomtuliza kimwili na kisaikolojia.
Mbali na kuwa ala ambayo inahitaji umakinifu katika ujifunzaji na uchezaji, sauti hujitokeza kulingana na namna unavyosongeza vidole wakati wa ‘kukata’ waya.
Anaamini katika kucheza ala hii, ataweza kufika mbali katika usanii na kugeuza zeze kuwa kitega-uchumi.
Kinachompa matumaini ni jinsi kikundi chao cha drama shuleni kinavyozidi kuimarika hatua kwa hatua kiasi cha kuwapa fursa za kuzuru sehemu nyinginezo.
Uraibu wake mwingine ni kuimba, kusoma, kusakata kandanda na kucheza mpira wa vikapu.
Joshua anawarai chipukizi wenye nia ya kujua kucheza chombo hiki kwamba, wanahitajika kuwa wazingativu na makini kwa sababu huhusisha saikolojia ya mchezaji. Pili, wafuate maelekezo ya mwelekezi ndiposa wajue jinsi ya ‘kukata’ waya kwa kufuata mdundo na mirindimo ya muziki wanaoucheza.
Subscribe our newsletter to stay updated