• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:47 PM
JAMVI: Onyo utawala wa Jubilee unarejesha Kenya gizani

JAMVI: Onyo utawala wa Jubilee unarejesha Kenya gizani

Wakili mbishi Dkt Miguna Miguna alipowasili jijini Toronto, Ontario, Canada baada ya kufurushwa humu nchini Februari 5, 2018. Picha/ Hisani

Na BENSON MATHEKA

Kwa Muhtasari:

  • Watetezi wa haki za binadamu wanaonya kwamba haki za binadamu zinapuuzwa ili kurejesha Kenya katika utawala wa kiimla wa chama cha KANU
  • Ingawa serikali ilisema kwamba Miguna alikuwa raia wa Canada, iliibuka kuwa walikataza maafisa wa ubalozi wa nchi hiyo jijini Nairobi kumuona
  • Gharama ya ukiukaji wa haki za binadamu ni kubwa. Wanaowajibika wanafaa kuheshimu katiba na kuwa msitari wa mbele kuilinda

MATUKIO yaliyopelekea kufurushwa kwa mwanasiasa mbishi Miguna Miguna yamefanya serikali kushutumiwa vikali na kuonywa dhidi ya kurejesha Kenya katika enzi za giza kwa kupuuza utawala wa sheria, kunyanyasa upinzani na kukiuka haki za raia.

Watetezi wa haki za binadamu na wanauchumi wanaonya kwamba hatua ambazo Kenya ilipiga chini ya katiba mpya hasa kuhusu haki za binadamu, zinapuuzwa kwa lengo la kurejesha Kenya ilivyokuwa chini ya utawala wa kiimla wa chama cha Kanu.

Wanasema dalili za Kenya kurejea katika enzi za giza zinajitokeza kufuatia kukandamizwa kwa vyombo vya habari, kukamatwa na kuzuiliwa kwa watu wanaokosoa serikali na kupuuzwa kwa maagizo ya mahakama.

 

Mwelekeo hatari

Kulingana na Tume ya Taifa ya Haki za Binadamu (KNHRC), serikali imechukua mwelekeo hatari unaoweza kutumbukiza nchi katika msukosuko kwa kutoheshimu utawala wa sheria.

KNHRC inataja ukadamizaji wa uhuru wa wanahabari na maafisa wa serikali na kudharau mahakama kama vitisho kwa utawala wa sheria, upuuzaji wa haki za binadamu na demokrasia.

“Tume inasikitishwa na matukio ya wiki moja iliyopita ambapo kumekuwa na ongezeko la visa vya kudharau utawala wa sheria, vitisho kwa haki za binadamu na haki za kidemokrasia ambazo zimetambuliwa na kuhifadhiwa katika katiba,” asema mwenyekiti wa tume hiyo, Bi Kagwiria Mbogori kwenye onyo kwa waziri wa usalama wa ndani, Dkt Fred Matiang’i, Inspekta Jenerali wa polisi Joseph Boinnet na ofisi ya mkurugenzi wa mashtaka ya umma.

Maafisa hao watatu walipigwa darubini kufuatia kukamatwa kwa viongozi wa upinzani, kuwapokonywa walinzi, silaha na paspoti zao na kuandamwa na maafisa wa polisi.

 

Enzi za giza

“Tunatoa onyo kwamba Kenya inarejea kwa haraka katika enzi za giza na zenye uchungu mwingi. Tunalaani vikali kukamatwa kiholela kwa watu na kudharau mahakama kunakoendelea,” asema Bw Mbogori.

Onyo hilo lilijiri saa chache baada ya serikali kumtimua mwanasiasa Miguna Miguna ikidai hakuwa raia wa Kenya baada ya kukamatwa na polisi na kuhangaishwa kwa siku tano.

Polisi walikataa kutii maagizo kadhaa ya mahakama kumfikisha kortini. Inspekta Jenerali wa polisi Joseph Boinnet na Mkurugenzi wa upelelezi George Kinoti pia walipuuza agizo la Jaji Luka Kimaru la kufika mbele yake kueleza kwa nini walikataa kutii agizo la mahakama.

Ingawa serikali ilisema kwamba Miguna alikuwa raia wa Canada, iliibuka kuwa walikataza maafisa wa ubalozi wa nchi hiyo jijini Nairobi kumuona akiwa seli hatua ambayo mawakili wanasema ni kilele cha ukatili.

 

Twaelekea wapi?

“Ikiwa polisi wanaweza kumkamata raia wa nchi ya kigeni na kunyima ubalozi wa nchi hiyo nafasi ya kumuona, tunafaa kujiuliza tunaelekea wapi kama nchi na kurekebisha mambo kabla ya kuharibika zaidi,” alisema wakili mmoja aliyeomba tusitaje jina lake kwa sababu ya uhusiano wake na Jubilee.

Anasema matukio ya hivi majuzi yanaonyesha kwamba washauri ambao rais anatengemea. Bi Mbogori anamtaka Bw Boinnet kuhakikisha polisi wanafuata katiba na kutimiza viwango vya haki za binadamu katika kazi yao.

“Agiza maafisa wote wa polisi kufuata katiba kikamilifu na kuheshimu haki za binadamu za watu wanaokamatwa na wote wanafaa kuchukuliwa kuwa sawa bila ubaguzi kwa misingi yoyote,” Bi Mbogori alimweleza Bw Boinnet.

KNHRC ilimwelekezea waziri Matiang’i kidole cha lawama kwa kukandamiza uhuru wa wanahabari na kumuonya kwamba maagizo anayotoa hayafai kukiuka katiba.

“Fuata sheria na ukome mara moja kutoa amri zinazoenda kinyume cha sheria,” tume ilimweleza Bw Matiang’i na kumtaka kufungua vituo vya runinga ilivyoagiza mahakama. Serikali ilifungua vituo vya NTV na KTN News lakini ikachelewa kufungua Citizen Tv na Inooro Tv.

 

Kusambaratisha uchumi

Wadadisi wanasema serikali ikiendelea kukandamiza upinzani, kudharau mahakama na kupuuza utawala wa sheria inaalika msukosuko ambao utalemaza ukuaji wa uchumi.

“Ni mwelekeo mbaya ambao utaathiri uchumi wa nchi, hakuna mwekezaji anayependa nchi isiyo thabiti kisiasa,” asema Dkt Rajnkat Shah, mwekezaji wa kimataifa.

Bi Mbogori anaonya kwamba hali ya kisiasa nchini inaathiri haki za vijana, wanawake, watoto, wazee na watu walio na ulemavu na tayari imeanza kuzua taharuki.

“Ripoti ya tume inaonyesha kuwa kufikia Februari 6, maandamano ya raia yemelipuka katika maeneo ya Kisumu na Migori ambapo mtu mmoja aliuawa Ahero, mali ikaharibiwa na kuibwa. Hali ya sasa inaonyesha jamii inayokumbwa na taharuki na kugawanyika kwa misingi ya kikabila na kisiasa,” anaeleza Bi Mbogori.

Anaonya kwamba maafisa wa serikali wanaohusika hawatajukumika, hali itakuwa mbaya zaidi na kuzaa majuto.

“Tume inawakumbusha wote wanaohusika kwamba gharama ya ukiukaji wa haki za binadamu ni kubwa, gharama ambayo nchi inayong’ang’ana kutimiza mahitaji yake ya kiuchumi na maslahi ya kimsingi ya raia wake haiwezi kumudu. Wanaowajibika wanafaa kuheshimu katiba na kuwa msitari wa mbele kuilinda na kuitetea kwa nia nzuri,” alisema

You can share this post!

JAMVI: Je, Mlima Kenya waweza kumuunga mkono Kalonzo...

JAMVI: Uhuru pabaya kwa kusahau baadhi ya maeneo ya Gema...

adminleo