Michezo

Droo ya Man City na Liverpool yamuacha ndovu juu ya mti

March 10th, 2024 2 min read

NA MWANGI MUIRURI 

DROO ya 1-1 kati ya Manchester City na Liverpool Jumapili jioni, Machi 10, 2024 ina maana kwamba timu ya Arsenal ndiyo kidedea katika jedwali la Ligi kuu ya Uingereza (EPL) kwa pointi 64.

Liverpool ni ya pili sasa ikiwa na pointi 64, lakini ikidunishwa na Arsenal kwa mabao 46 dhidi ya 39.

Nayo Man City iko katika nafasi ya tatu kwa pointi 63, wote wakiwa wamecheza mechi 28, mkabano ukizidi kutesa na kusisimua miongoni mwa timu hizo tatu.

Mtanange huo wa Man City na Liverpool uligeuka kuwa wa kutikisa ndovu ambayo ni Arsenal kutoka juu ya mti.

Dakika ya 23 ndovu aliteremshwa hadi nafasi ya pili na bao la Liverpool kutoka kwa John Stones, lakini bao la Man City kupitia penalti ya Mac Allister kunako dakika ya 50 likarejesha ndovu tena juu ya mti.

Mashabiki wa Man United na Chelsea walikuwa wakiomba kwa unyenyekevu wa kutisha Arsenal ishuke hadi chini ya meza ambako wao wamekuwa wenyeji bila matumaini ya kupaa.

Mkabano ulizidi kuvuma kati ya Man City na Liverpool jinsi muda ulivyozidi kuyoyoma.

Mtanange ukielekea dakika za 60, Liverpool ilikuwa ikionekana wazi ikiwa na nia ya kuibuka na ushindi.

Ni katika hali hiyo ya hofu ambapo shabiki sugu wa Arsenal, Askofu Danson Gichuhi almaarufu Askofu Yohana wa kutoa wanawake mapepo kupitia kuwapaka mafuta maalum alisema kwamba unabii wake haukuwa umefunuliwa kuhusu ni nani angetwaa ushindi.

Aliwataka wenzake wa Arsenal wakaze na maombi mtanange uishe droo, na ikiwa walitii na wakaomba iwe hivyo, basi yalijibiwa kwa utamu walioutaka.

Dakika za lala salama Liverpool iliamsha makali ya maangamizi.

Ndovu naye akiwa juu ya mti ikawa kwake ni kiwewe.

Refarii aliposema dakika za ziara zilikuwa 8, wafuasi wa Arsenal waliona kama ni hujuma, lakini wakashikilia nyoyo zao kwa kujikaza na sasa kipenga cha mwisho kilipopulizwa mechi ikaishia droo.

Takwimu za mechi zilikuwa Liverpool ikiwa na mashuti 19 ya kuelekea michumani dhidi ya 10 ya Man City, huku yaliyolenga lango yakiwa ni 6 kwa 6.

Umiliki wa mpira uliwaendea Liverpool kwa asilimia 53 dhidi ya 47, pasi za Man City zikiwa 510 dhidi ya 565 na zikiwa na uhakika wa asilimia 81 dhidi ya 84 mtawalia.

Liverpool ilicheza ngware 6 dhidi ya 10 za Man City na ambazo ziliishia vijana hao wa Man City kuonyeshwa kadi tatu za majano.

Liverpool wakinolewa na Jurgen Klopp waliotea mara 6 dhidi ya hao Man City ya Pep Gardiola ambapo walijenga kibanda kwa wenyewe ugani Anfield bila idhini mara moja tu.

Liverpool ilipata Kona 7 dhidi ya 4, bao la Liverpool likitokea kupitia penati hiyo moja ya kipekee.

[email protected]