• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 1:50 PM
ANC sasa yamkabidhi Rais Zuma barua rasmi ya kumtaka ang’atuke mamlakani

ANC sasa yamkabidhi Rais Zuma barua rasmi ya kumtaka ang’atuke mamlakani

Na AFP

PRETORIA, AFRIKA KUSINI

Kwa Muhtasari:

  • Ikiwa Zuma, atapuuza wito wa kung’atuka mamlakani, atang’olewa kupitia kura ya kutokuwa na imani naye bungeni
  • Zuma ameomba muda wa miezi mitatu kung’atuka mamlakani
  • Ripoti tofauti zilidai Rais Zuma alimjibu Ramaphosa: “Nifanyie unachotaka lakini sibanduki”
  • Uchumi wa Afrika Kusini umedorora wakati wa utawala wake

CHAMA tawala cha African National Congress (ANC), sasa kimemkabidhi rasmi Rais Jacob Zuma barua ya kumtaka ajiuzulu. Uongozi wa ANC ulimtaka kung’atuka baada ya viongozi wa ngazi za juu kukutana Jumanne asubuhi.

Ikiwa Rais Zuma, 75, atapuuza wito wa chama cha ANC kung’atuka mamlakani, atang’olewa kupitia kura ya kutokuwa na imani naye bungeni.

Viongozi na wabunge wa ANC wanatarajiwa kukutana leo katika majengo ya bunge ili kujadili hatua itakayochukuliwa dhidi ya Rais Zuma baada ya kukaidi agizo la kumtaka kung’atuka.

Rais Zuma ambaye amekuwa akiongoza Afrika Kusini tangu 2009 anakabiliwa na sakata mbalimbali za ufisadi.

Tangu naibu wake Cyril Ramaphosa kuchaguliwa kuwa kiongozi wa ANC Desemba, mwaka jana, Rais Zuma amekuwa akishinikizwa kujiuzulu.

 

Barua

Katibu Mkuu wa ANC Ace Magashule Jumanne alimpelekea Rais Zuma barua ya kumtaka kujiuzulu katika Ikulu ya Rais jijini Pretoria.

Hata hivyo, jibu la Rais Zuma kwa Bw Magashule halikujilikana mara moja. Viongozi wa ANC Jumatatu walikutana kwa zaidi ya saa 13 ambapo waliafikiana Rais Zuma ang’atuke.

Katika mkutano huo wa Jumatatu, Rais Zuma na makamu wake Ramaphosa walijibizana kwa hasira hadharani.

Shirika la habari la serikali, SABC, liliripoti kuwa Bw Ramaphosa alimpa Rais Zuma muda wa saa 48 kujiuzulu.

Lakini wanachama wa ANC wanaounga mkono Rais Zuma wanasema kuwa kiongozi huyo hatajiuzulu kabla ya muhula wake kukamilika mwaka ujao.

Baadhi ya vyombo vya habari pia viliripoti kuwa Rais Zuma ameomba muda wa miezi mitatu kung’atuka mamlakani.

 

‘Sibanduki’

Ripoti tofauti zilidai Rais Zuma alimjibu Ramaphosa: “Nifanyie unachotaka lakini sibanduki”.

Msemaji wa Zuma jana alikataa kuzungumza na wanahabari huku mwanawe, Edward, akisema kuwa atazungumza baada ya chama cha ANC kutoa uamuzi wake wa mwisho.

Ijumaa, mmoja wa wake wa Zuma, Tobeka Madiba-Zuma, aliandika katika mtandao wa Instagram kuwa mumewe yuko tayari kupigana hadi mwisho badala ya kujiuzulu.

Bi Tobeka Madiba-Zuma hata alishutumu mataifa ya Magharibi kuwa kuunda njama ya kutaka kumng’oa mamlakani Rais Zuma.

“Atakamilisha miradi aliyoanzisha na hatakubali maagizo kutoka kwa mataifa ya kigeni,” akasema.

Uchumi wa Afrika Kusini umedorora wakati wa utawala wa Rais Zuma huku serikali yake ikikumbwa na sakata za ufisadi kila uchao.

You can share this post!

Maandalizi ya Stars U-20 yakosa kung’oa nanga tena

Kituo cha redio cha Kikristo chafungwa kudunisha wake

adminleo