• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
JARED OUNDO: Anahakikisha vijana wamesalia nguzo ya jamii

JARED OUNDO: Anahakikisha vijana wamesalia nguzo ya jamii

NA PAULINE ONGAJI

Alianza kujihusisha na masuala ya kunasihi vijana akiwa katika kidato cha pili na miaka kumi baadaye mchango wake katika kuimarisha maisha ya vijana unahisiwa katika fani mbalimbali katika jamii.

Huo ulikuwa mwaka wa 2008 ambapo Jared Oundo, 26, wakati huo akiwa katika kidato cha pili, alizamisha akili yake katika masuala ya kusaidia jamii na hasa vijana huku akianzisha shirika la Jubilant Stewards of Africa.

Ni mwito ambao aliuendesha hata baada ya kukamilisha shule ya upili ambapo katika kipindi cha mwaka mmoja pekee alisajili shirika hili na kuanza rasmi kunasihi vijana kuhusu jinsi ya kufanya vyema shuleni, kuwahamasisha kuhusu athari za matumizi ya mihadarati na jinsi ya kukabiliana na virusi vya HIV, umuhimu wa kutangamana na watu, miongoni mwa mambo mengine.

Kufikia sasa, anajivunia kuendesha shughuli hii katika mataifa 23 barani Afrika ikiwa ni pamoja na Kenya, Sierra Leone, Zambia, Afrika Kusini, Zimbabwe, Malawi na Sudan Kusini.

Bw Oundo akihutubia wanafunzi wa Taasisi ya Uzuri. Picha/ Hisani

Kadhalika ameshiriki katika kuanzisha vyama katika shule za msingi na upili na vyuo vikuu ambapo anatumia jukwaa hili kunasihi wanafunzi. “Hapa ndipo suala la kufanya vyema masomoni, vile vile jinsi ya kuchagua taaluma zinazowafaa huzungumziwa,” aeleza.

Shughuli zizi zimempeleka katika mamia ya taasisi za kielimu katika Kaunti mbalimbali. “Baadhi ya taasisi hizo ni pamoja na shule za upili za Highway, Moi Girls, Upperhill School, Ruai Boys (Nairobi); shule za msingi kama vile Buyende Primary School, Kaunti ya Busia, na Chuo Kikuu cha Masai Mara, miongoni mwa taasisi zingine,” aeleza.

Ni ujumbe huu unaopitishwa kupitia kitabu chake Awakening the Academic Giant kinachohimiza wanafunzi kuimarisha matokeo yao shuleni. Kupitia jitihada hizi wanafunzi wengi ambao awali walikuwa na alama za chini shuleni wamezidi kuimarika.

Kampeni zake hazijakomea tu hapo kwani amejihusisha vilivyo katika vita dhidi ya maradhi ya zinaa na hasa virusi vya HIV. “Nimehusika katika vikao vya kuwashauri vijana, kuwahamasisha kuhusu maradhi ya zinaa na mbinu za kuhakikisha usalama wao,” aeleza.

Bw Oundo akiwashauri wanafunzi wa shule ya upili. Picha/ Hisani

Mafunzo haya yameendelezwa katika sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na vitongoji duni kadha jijini Nairobi kama vile Mukuru Kwa Reuben, Kwa Njenga na Kayole. Pia wameendesha shughuli hizi katika Kaunti za Uasin Gishu, Kisumu, Busia, Meru, Narok na Homa Bay miongoni mwa zingine, ambapo pia madhumuni ni kukabiliana na tatizo la unyanyapaa kwa wale ambao tayari wana virusi hivi.

Mradi huu ulianza kama chama kidogo pindi baada ya kuondoka sekondari huku ari yake ikichochewa na aliyekuwa Rais wa Amerika Barack Obama na mwanaharakati wa mazingira, marehemu Prof Wangari Maathai. “Nilishuhudia vijana wengi wakitaabika kwani walikuwa wametekwa na mihadarati, na hivyo nikatumia nafasi hiyo kukuza ndoto zao,” aeleza.

Lakini sasa japo anahisi kwamba hajaafikia lengo lake, kupitia jitihada zake vijana wengi wamebadilisha mienendo kwani visa vya ulevi, matumizi ya mihadarati, mimba za mapema na maambukizi ya virusi vya HIV vimepungua.

Kwa sasa ndoto yake ni kuona bara la Afrika likikuza vijana wanaowajibika na watakaochukua uongozi katika siku zijazo na hivyo kuimarisha maisha ya raia wa bara hili.

You can share this post!

Matamshi ya Murathe yaipasua Jubilee

AKILIMALI: Teknolojia mpya ya kukuza viazi inavyowapunguzia...

adminleo