Habari za Kitaifa

Korti yapunguza presha ya kumtimua Gachagua


KIONGOZI mmoja wa vijana katika kaunti ya Laikipia amewasilisha kesi katika Mahakama Kuu ya Nyahururu akitaka kuzuia Bunge la Kitaifa kuwasilisha au kujadili hoja ya kumuondoa madarakani Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Na wakati huo huo, Mahakama Kuu imezuia polisi na Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) kuwakamata na kuwafungulia mashtaka washirika wanne na wasaidizi wa Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Jaji wa Mahakama ya Juu Lawrence Mugambi aliidhinisha kuwa ya dharura kesi iliyowasilishwa na aliyekuwa mbunge wa Nyeri Mjini Bw Ngunjiri Wambugu, George Theuri na Pius Munene, kuwa ya dharura na akatoa agizo kuzuia kukamatwa kwao au kufikishwa mahakamani, kusubiri kuamuliwa kwa kesi yao.

Katika kesi tofauti, wabunge Bw Benjamin Gathiru Mwangi almaarufu Mejja Donk (Mbunge wa Embakasi ya Kati), James Gakuya (Embakasi Kaskazini), walipata maagizo ya mahakama ya kuzuia kukamatwa kwao.

Katika Mahakama ya Nyahururu Bw Denis Ndereva, Mkurugenzi Mkuu shirika la Youth for Youth Africa, pia anataka agizo la Mahakama kuzuia Bunge la Kitaifa na Seneti kujadili hoja yoyote ya kumuondoa mamlakani Naibu Rais hadi atakapomaliza muhula wake.

Kesi hiyo imetaja Bunge la Kitaifa kama mshtakiwa wa kwanza, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula kama mshtakiwa wa pili, Spika wa Seneti Amason Kingi kuwa mshtakiwa wa tatu, na Mwanasheria Mkuu ni mshtakiwa wa nne.

Chini ya cheti cha dharura, Bw Ndereva anadai hoja ya kumtimua Gachagua ambayo inapanga kuwasilishwa imechochewa kisiasa, inakiuka taratibu za kikatiba.

‘Mlalamishi anaibua masuala kadhaa ya kisheria ili mahakama iamue, ikiwa ni pamoja na ikiwa hoja ya kumtimua Naibu Rais Geoffrey Rigathi Gachagua inatimiza kiwango cha katiba kama ilivyoainishwa katika Kifungu cha 150 cha Katiba ya Kenya 2010,’ anasema katika kesi yake.

Anataka mahakama iamue iwapo mchakato wa kumuondoa Gachagua mamlakani unakiuka kanuni za haki, haki asilia, utaratibu unaostahili na kuingiliana kwa mamlaka.

Bw Ndereva pia anaitaka mahakama kubaini iwapo ana haki ya kupewa amri ya kudumu ya kuzuia majaribio yoyote ya baadaye ya kumshtaki Naibu Rais.

Anasema kuwa Katiba inatoa misingi mahususi ya kuondolewa ofisini kwa Naibu Rais ikiwa ni pamoja na ukiukaji mkubwa wa Katiba, kutenda uhalifu, utovu wa nidhamu uliokithiri, au kutokuwa na uwezo wa kufanya kazi rasmi.

“Mlalamishi anasema kuwa hoja ya kumshtaki haikidhi matakwa magumu yaliyoainishwa katika Katiba. Hoja hiyo, kama ilivyoandaliwa, haina msingi wa wazi wa kisheria na inaendeshwa na ushindani wa kisiasa badala ya vigezo halali vya kikatiba,” anasema.

Bw Ndereva anasema kuwa mchakato huo umechochewa kisiasa na ni matumizi mabaya ya mamlaka ya bunge.

“Mlalamishi anaomba ulinzi kutoka kwa mahakama hii ili kuzuia matumizi mabaya ya mamlaka ya bunge na kulinda haki za kikatiba za Naibu Rais Rigathi Gachagua. Mchakato wa kumuondoa ofisini, kama ulivyoanzishwa sasa, unakiuka Katiba na unadhoofisha misingi ya haki, uadilifu na utawala wa sheria,” anasema katika kesi yake.

Hasa anaitaka mahakama kutoa maagizo anayoomba ili kuhakikisha kuwa majaribio yoyote ya baadaye ya kuondoa naibu rais yanazingatia miongozo ya kikatiba.