Makala

Sura mpya ya upinzani Kenya yamkosa Raila baada ya miaka mingi

Na BENSON MATHEKA June 6th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

UKURUBA unaoimarika kila siku kati ya Rais William Ruto na kiongozi wa ODM, Raila Odinga, umeanza kubadilisha sura ya upinzani Kenya.

Kwa miaka mingi, Raila amekuwa nembo ya upinzani Kenya, jukumu ambalo anaonekana kutema kufuatia ushirikiano wake na serikali ya sasa ya Kenya Kwanza na iliyotangulia ya Jubilee.

Raila na Ruto, ambao kwa muda mrefu wamekuwa mahasimu wakubwa wa kisiasa, sasa wanashirikiana katika hali ambayo haikutarajiwa, hasa baada ya kushindana vikali katika uchaguzi mkuu wa 2022.

Kwa wengi, ushirikiano huu unazua maswali kuhusu lengo lao.

Na ushirikiano wao ukiendelea kuimarika kila uchao, sura mpya za upinzani zinajitokeza na muungano mpya wa upinzani unaanza kusukwa ukishirikisha Martha Karua, Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa na Fred Matiang’i.

Wengine wanaojitokeza kama sura ya upinzani kwa wakati huu ni aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga, Mbunge wa Mumias Mashariki Peter Salasya, waliokuwa mawaziri Justin Muturi, Mithika Linturi na gavana wa Trans Nzoia, George Natembeya.

Seneta wa Busia Okiya Omtatah ambaye amekuwa mwanaharakati wa kutetea wanyonge sasa anaonekana kujiunga na upinzani wa kisiasa huku akikosoa serikali kwa sera zake.

Karua na Gachagua, ambao walikuwa wagombea wenza wa miungano tofauti mnamo 2022, sasa wanaonyesha nia ya kushirikiana.

“Ninatarajia kushirikiana na wewe, Gachagua. Hatutaruhusu Rais Ruto kuwa dikteta,” alisema Karua katika mkutano wa hadhara mwezi jana.

Kwa wengi, ushirikiano wa Raila na Ruto umebadili sura ya upinzani. Huku wachache wakiutazama kama mkakati wa busara, wengine wanasema ni usaliti wa misingi ya kidemokrasia.

Muungano huu ulianza kuchukua sura wakati Rais Ruto alimuunga mkono Raila kugombea uenyekiti wa Tume ya Muungano wa Afrika.

Ingawa Raila alishindwa katika azma hiyo, hatua hiyo ilizalisha uhusiano wa karibu kati ya viongozi hao wawili na ndipo viongozi wapya wa upinzani walianza kujitokeza.

“Mkakati wa Ruto ulikuwa wazi. Alitaka kumuondoa Raila katika siasa za kitaifa hadi bara la Afrika, na kwa kufanya hivi angerithi kura za ngome yake,” asema mchambuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.

Kwa kufanya hivi, asema, Ruto alipangua upinzani kwa weledi.

Hata hivyo, maandamano ya kizazi cha Gen Z yaliyotikisa serikali ya Ruto mwaka uliopita, yalibadilisha kila kitu.

Wakati presha ya kisiasa iliongezeka, Ruto alimwendea Raila kuomba usaidizi kutoka kwa ODM kwa kubadilishana nyadhifa serikalini.

Pia, kulikuwa na suala ya kupata idadi ya wabunge wa kumtimua aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ambaye sasa amegeuka kuwa sauti kubwa katika upinzani.

Hata hivyo, muungano huo unatiliwa shaka. Wakosoaji, akiwemo Rais Ruto, wanasema hauna ajenda huku baadhi wakihoji kama watu wenye misimamo tofauti wanaweza kushirikiana.

Gachagua anajibu akisema: “Ajenda yetu ya kwanza ni kuhakikisha Ruto anakuwa rais wa muhula mmoja,” alisema hivi majuzi katika mkutano wa kisiasa huko Machakos, huku upinzani ukijitahidi kuonyesha umoja.

Baadhi ya wadadisi wanataja hatua ya Raila kujitenga na upinzani kama usaliti wa misingi ya kidemokrasia.

Raila mwenyewe ameanza kuisifu serikali ya Kenya Kwanza kwa kile anachotaja kama kutekeleza baadhi ya sera za uliokuwa muungano wa Azimio La Umoja One Kenya.

Katika ziara ambazo aliandama na Ruto Homa Bay, alisema: “Yote haya yalikuwa sehemu ya mipango yetu ya Azimio. Kenya Kwanza wameiga, na hilo ni jambo jema.”

“Mtu anaweza kusema kwa urahisi kuwa Raila anasaidia kuendeleza ukatili dhidi ya raia. Hauwezi kupigana na nguruwe kwenye tope na utoke ukiwa safi,” alisema aliyekuwa waziri, Justin Muturi, ambaye alifutwa kazi baada ya kuikosoa serikali kuhusu utekaji nyara.