‘Yaya’ anayemiliki kiwanda cha kuuza mimea asili ng’ambo
ESTHER Ngina ni mwasisi wa Taste Kenya Exporters, kampuni inayouza mimea asilia ng’ambo ambaye hadithi yake inatia motisha – hakuna lisilowezekana kupitia bidii.
Aliingilia biashara ya uuzaji wa mimea ya kiasili, ndiyo herbs kwa Kiingereza, baada ya kuhudumu katika sekta ya maua.
Licha ya kuwa na Stashahada ya Usimamizi wa Masoko, safari ya Esther haikuanza kwa urahisi.
Wakati mmoja – akiwa katika shule ya upili, anafichua kwamba alifanya kazi kama yaya ili kugharamia karo yake.
Hata baada ya kuandika Mtihani wa Kitaifa Kidato cha Nne (KCSE), aliendelea na kazi hiyo hadi akafanikiwa kukusanya hela kuondoa malimbikizo ya karo ili aweze kujiunga na taasisi ya juu ya masomo.

“Mwajiri wangu, alijitolea kunisomesha nikapata Stashahada,” anasema.
Baada ya kuhitimu, Esther anadokeza kwamba alipata nafasi ya kazi katika kampuni ya kuuza maua nje ya nchi. Mwanya huo, ulimfumbua macho.
Alikuwa akisafiri na bosi wake nchi mbalimbali, na anasema safari ya kufikia alipo sasa ilishawishiwa na wateja aliokutana nao.
“Kampuni niliyofanyia kazi ilijishirikisha na uuzaji wa maua, na wateja wengi walikuwa wakiulizia mimea asilia kama vile mint na rosemary,” Esther anaelezea.
Swali hilo lilimpa wazo la uwekezaji.
Mwaka 2012, licha ya changamoto za kifamilia ikiwemo kupoteza mama yake, Esther alikata kauli ya kuacha kazi na kufukuzana na wazo jipya alililopata.
Anadokeza kuwa maamuzi hayo aliyafanya akiwa na miaka 30, umri ambao kwa wengi ni muhimu sana kujituma kusaka mianya tele ya ufanisi kupitia ajira.

Hata hivyo, kwake hilo halikuwa hoja. Aliamua – na liwe liwalo, ataingilia biashara angaa naye pia awe mwajiri.
Mtaji, haukuwa kikwazo vile kwani alikuwa amejiunga na chama cha ushirika kuweka akiba.
“Nilichukua mkopo wa Sh1.2 milioni,” Esther anasema.
“Nilianza kwa kushirikiana na marafiki wachache kusafirisha bidhaa kama vile French beans na snow peas ng’ambo,” anaongeza.
Baadaye, walijumuisha mimea ya kiasili kama coriander, thyme, na dill.
Changamoto hazikukosekana. Kukosa mtaji wa kutosha kupanua biashara na ujuzi wa usimamizi kulimlazimu kuuza asilimia 25 ya hisa za biashara yake ili kujisimamia.
Akiendelea tu kuboresha biashara, Esther anafichua kwamba aliwahi pia kupoteza shamba la ekari 10 – la kukodi lililokuwa na vivungulio 31, eneo maalum la kupakia mazao na ofisi, kutokana na mmiliki aliyetamatisha makubaliano ya kandarasi kabla muda kukamilika. Hakukata tamaa.

Alianzisha kampuni tanzu kama Herbspice Market Link Ltd, inayoshughulika na wakulima wa mashamba madogo wanaomsambazia mazao kusafirisha ng’ambo, na Makena Paradise Herbs Ltd inayolenga kuongeza bidhaa thamani, iliyopewa jina la binti yake.
Mengine yamekuwa historia, Taste Kenya Exporters sasa ikiwa kati ya kampuni zinazoletea Kenya mapato kupitia uuzaji wa bidhaa za shambani ughaibuni.
Katika shamba lake la robo ekari lililoko Enkasiti, Kajiado, ana kivungulio cha kuoteshea miche ya mimea asilia kama rosemary na oregano.
Akiwa na leseni kutoka kwa taasisi ya Mbegu na Ustawishaji wa Mimea Nchini (Kephis) mjasiriamali mali huyu huagiza mbegu kutoka Uhispania, Italia, na Uingereza.
“Huotesha miche mara mbili kwa mwezi, na ninakadiria kuzalisha zaidi ya miche 200,000 ninayouza kati ya Sh2 hadi Sh8 kila mche,” akaambia Akilimali wakati wa mahojiano.

Ni hatua anayosifia kuokoa wakuzaji wa mimea asilia, ikizingangatiwa kuwa mbegu zake ni bei ghali.
Aidha, Esther anashirikiana na wakulima wapatao 400 kutoka maeneo mbalimbali ya nchi kama vile Nairobi, Machakos, Laikipia na Kajiado.
Huwasambazia miche na pia kuwasaidia kuuza mazao masoko ya ng’ambo.
Taste Kenya Exporters inalenga masoko ya Ulaya – nchi kama Uholanzi na Ujerumani, pamoja na mataifa ya Milki za Kiarabu (UAE) na Saudi Arabia.
“Kwa wasio na kampuni, huwauzia moja kwa moja kupitia kampuni yangu ambayo ina kibali na wenye kampuni ila hawaelewi taratibu huwasaidia kimikakati,” anasema.
Kwa sasa, mama huyu wa watoto wawili ameajiri wafanyakazi 20, akiwemo mtaalamu wa masuala ya kilimo, na anaendelea kupanua uwekezaji wake, akihimiza vijana kuwekeza muda na maarifa yao katika ujasiriamali.
