Maandamano ya Gen Z: Bunge laahirisha kikao
BUNGE la Kitaifa jana lililazimika kuahirisha kikao chake cha asubuhi kufuatia ukosefu idadi tosha ya wabunge kuliwezesha kuendesha shughuli zake.
Spika wa muda David Ochieng aliamuru kuahirishwa kwa kikao hicho saa tano na dakika 45 baada ya kubainika kuwa ni wabunge 10 pekee waliokuwa ukumbini.
“Ikiwa zimesalia dakika 15 kabla ya saa sita, kikao cha bunge hili kimeahirishwa hadi saa nane na nusu alasiri leo hii,” Bw Ochieng’ ambaye ni Mbunge wa Ugenya, akaamuru.
Kikao cha jana kilianza saa tatu na nusu asubuhi wakati ambapo maandamano ya kuadhaminisha mwaka mmoja tangu kuuawa kwa Gen Z Juni 25, 2024 kuanza jijini Nairobi na maeneo mengine ya nchi.
Ni siku hiyo ambapo waandamanaji walivamia majengo ya bunge, hali iliyochangia wabunge kutoroka kuokoa maisha yao.
Dakika chache baada ya Bw Ochieng’ kuahirisha kikao cha asubuhi cha Jumatano, magari ya wabunge yalionekana yakiondoka maeneo ya maegesho ishara kuwa wabunge waliingiwa na wasiwasi kuhusu usalama wao.
Kamati mbili za bunge la kitaifa ambazo zilikuwa zimeratibiwa kufanya vikao Jumatano pia zilikazimika kuahirisha vikao hivyo.
Hii ni kutokana na usalama mkali ambao ulikuwa umewekwa ndani na nje ya majengo ya Bunge baada ya familia za waathiriwa wa maandamano ya mwaka jana kuahidi kufika hapo kuwasilisha taarifa ya malalamishi yao.
Kamati ya Kuhusu Uwezekezaji kuhusu Elimu na Utawala, inayoongozwa na Mbunge wa Bumula Jack Wambuka, iliahirisha kikao kutokana na hofu kuhusu usalama.
Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Mazingira, inayoongozwa na Mbunge wa Mwala Vincent Musyoka Kawaya, pia ilifeli kufanya kikao chake Jumatano kutokana na sababu hizo hizo za kiusalama.