SARUFI: Makosa katika uandishi wa baadhi ya nomino ambazo zimeswahilishwa
LUGHA ya Kiswahili kama zilivyo lugha nyingine huwa na njia mbalimbali za kupata msamiati wake.
Mojawapo ya njia za kuunda nomino za Kiswahili ni uswahilishaji au utohozi.
Baadhi ya maneno ya Kiswahili yametoholewa kutoka kwa lugha nyingine kama vile Kiingereza.
Utohozi hasa hutokana na ukosefu wa msamiati fulani katika mazingira ya Kiswahili ama kubuniwa kwa vifaa vipya vya kiteknolojia ambayo vina majina ya lugha nyingine.
Wapo baadhi ya wanafunzi ambao wana changamoto wanapoyaandika maneno yaliyoswahilishwa.
Mara kwa mara utapata sentensi kama vile: *Nilienda kwa shangazi yangu kusherehekea Sikukuu ya Crisimasi. *Jana nilisikiliza mjadala kwenye radio.
*Abiria alipolipa nauli utingo alimpa ticketi.
Sentensi hizi zimetoholewa maneno visivyofaa. Mwandishi amekosa kuondoa baadhi ya herufi zinazotumiwa kuandika maneno haya kwa lugha ya Kiingereza.
Neno Crisimasi halifai kuwa na herufi c baada ya kuswahilishwa. Tunafaa kusema: Nilienda kwa shangazi yangu kusherehekea Sikukuu ya Krisimasi.
Neno *radio linafaa kuwa redio. Pia tunafaa kusema: Abiria alipolipa nauli utingo alimpa tiketi.
Aidha, wapo wanafunzi wenye mazoea ya kuandika maneno:
*Chocoleti badala ya chokoleti, paspoti badala ya pasipoti, *compyuta badala ya kompyuta, *Penceli padala ya penseli.
Mwanafunzi mwenye changamoto ya kuyaandika maneno yanayotokana na utohozi anafaa atambue silabi zinazotumiwa kuandika kila neno linalomtatiza.
Baada ya hapo, afanye mazoezi ya kuandika maneno hayo. Anaweza kutunga sentensi sahihi akitumia maneno yaliyotoholewa kwa usahihi ili kuimarisha mawasiliano yake.