Anasema heri akose hela kuliko kuuzia umma asali ya ubora wa chini
UUZAJI asali ni mojawapo ya biashara zinazoshuhudia utapeli mkubwa wa bidhaa, haswa kufuatia ongezeko la visa vinavyoripotiwa kuhusu mbinu nyingine zisizofaa zinazotumika wakati wa uchakataji wake.
‘Uchafuzi’ wa asali, huanzia kwa baadhi ya wafugaji na kuendelezwa na wafanyabiashara.
Kwa wanaoendeleza biashara hiyo kwa uaminifu, imani imekosekana kabisa hivyo basi kuwaweka kwenye njiapanda kushawishi wateja.
Hata hivyo, wapo wachache ambao wameapa liwe liwalo hawatachafua bidhaa hiyo, na msimamo wao umeanza kuzaa matunda.
Diana Ngui, mfugaji wa nyuki kutoka Kaunti ya Makueni, anapotazama cheti alichopokezwa pamoja na kombe alilotunukiwa mwaka jana na Shirika la Kutathmini Ubora wa Viwango vya Bidhaa Kenya (Kebs), utambuzi huo unampa motisha zaidi kuendelea kuinua viwango katika kazi yake.
Oktoba 2025, alitangazwa kuwa mzalishaji bora wa asali nchini, tuzo iliyothibitisha kuwa mbinu zake za ufugaji nyuki, usafirishaji na uchakataji wa asali zimekuwa sahihi.
Akiwa mwanzilishi wa Amaridina Honey, Diana hakufikia tu viwango vya kitaifa bali alivipita.
Wafanyabiashara matapeli wamekuwa wakishutumiwa kuchanganya asali na sharubati ya sukari, ndizi, molasi na viungio vingine vinavyoharibu ubora wa bidhaa hiyo ya nyuki.
“Cheti hiki cha shukrani kinatolewa kwa Amaridina Enterprise kwa kushiriki katika Tuzo za Ubora za Kenya 2025,” inaeleza sehemu ya cheti alichopewa Oktoba 24, 2025 na Mkurugenzi wa Kebs.
Kulingana na Diana, Kebs ilifanya uchunguzi wa kina wa sampuli za asali yake. Sampuli zilichukuliwa moja kwa moja kutoka kwenye mizinga shambani, katika kituo chake cha uchakataji na hata kwenye maduka ya rejareja kabla ya kutolewa kwa matokeo ya mwisho.
Matokeo yalikuwa sawa kila mahali: asali safi, isiyoharibiwa na yenye ubora unaofanana.
Katika sekta ambayo imekumbwa na visa vingi vya asali bandia au iliyochanganywa na vitu vingine, uthabiti huo ulimtofautisha na wengine.
Utambuzi huo, unaodumu kwa mwaka mmoja, ulimweka mfugaji huyo wa Makueni kileleni mwa wazalishaji asali bora Kenya.
“Nyuki hutengeneza asali bora kabisa. Ni binadamu ndio huiharibu kwa kuichakachua,” anasema Diana.
Safari yake katika ufugaji nyuki haikuanza na makumi ya mizinga.
Mwaka 2023, anadokeza kwamba alianza na mizinga mitano tu katika shamba lake la ekari tisa huko Makueni ambako pia anakuza nafaka.
Wakati huo, alipiga jeki kiwango chake cha asali kwa kununua kutoka kwa wakulima majirani.
Awali, alikuwa akisambaza sokoni kilo 20 za asali kwa mwezi. Kadri muda ulivyozidi kusonga, biashara yake ilikua na kustawi.
Kila baada ya miezi mitatu, mizinga yake ilianza kutoa karibu kilo 50 za asali, huku kila mzinga ukizalisha kati ya kilo nane hadi 10.
Miaka miwili baadaye, idadi ya mizinga yake imeongezeka hadi 20. Leo hii, huuza zaidi ya kilo 100 za asali kila mwezi; ambayo haijaongezwa thamani na iliyochakatwa, kwa wauzaji wa rejareja jijini Nairobi na kaunti jirani.
Hata hivyo, anakiri kuwa bado ni vigumu kukidhi mahitaji ya soko licha ya kushirikiana na wafugaji nyuki wengine wanaomsambazia asali.
“Ubora wa asali ndio unaodumisha wateja sokoni,” anasema.
Sekta ya asali nchini Kenya inaashiria pengo kama hilo. Kulingana na Idara ya Maendeleo ya Mifugo, Kenya ina uwezo kuzalisha hadi tani 100,000 za asali kwa mwaka.
Hata hivyo uzalishaji halisi ni karibu tani 17,000 pekee, hivyo kuacha pengo la tani 83,000.
Kwa kuwa matumizi ya kitaifa ni karibu tani 47,000 kwa mwaka, nchi hulazimika kuagiza asali kutoka nje kuziba upungufu wa takriban tani 30,000.
Kwa wazalishaji kama Diana, hii inaonyesha pengo kubwa lakini pia wajibu wa kudumisha viwango vya ubora unapaswa kutiliwa maanani.
Anasema mafanikio yake yanatokana na kufuata kwa makini taratibu za ubora kuanzia uvunaji, usafirishaji hadi uchakataji.
Haipashi asali joto kupita kiasi wala kuongeza molasi, sharubati ya sukari au ndizi ili kuongeza kiwango.
“Ningependelea nisiuze chochote, na mteja asubiri asali safi kuliko kuichakachua na kupoteza imani yake,” anasisitiza.
Ili kuhakikisha ubora, yeye husimamia hata uvunaji wa asali kutoka kwa wakulima wanaomsambazia.
Mbali na uzalishaji wa asali, Diana pia hutengeneza bidhaa nyingine kama mafuta ya mwili, lip balm propolis, kwa kutumia nta ya nyuki.
Hata hivyo anakiri kuwa safari yake haijakuwa rahisi.
“Kwa sababu ya visa vingi vya uchakachuaji wa asali sokoni, baadhi ya wateja hutilia shaka asali yangu.”