Changamoto na baraka za mvua kwa wazalishaji maziwa
MVUA imeanza kushuhudiwa katika sehemu nyingi za nchi, huku baadhi ya maeneo yakipokea kiasi kikubwa na hata kushuhudia mafuriko.
Mvua ni baraka kwa wakulima weng, kwani kwa sasa inaashiria kwamba msimu wa kupanda umefika na vilevile mifugo watapata malisho ya kutosha kwa muda mrefu.
Ezekiel Sang ambaye ni mkulima na mmoja wa viongozi wa Kaplesa Cooperative Society, eneo la Ziwa, Kaunti ya Uasin Gishu, anasema ukipiga darubini katika sehemu nyingi vijijini, wakulima hulisha ng’ombe au mbuzi kwa kutumia malisho ya kiasili kama vile nyasi za kawaida ambazo hazina virutubisho vya kutosha na aghalabu hupatikana kwa wingi msimu wa mvua nyingi.
“Malisho yaliyo mengi hapa nchini ni ya asili ambayo hutegemewa na mifugo. Hukomaa na kukauka mapema zaidi, na hivyo kusababisha lishe kwa wanyama kukosekana au kuwa duni,” asema.
Ndiposa wakati wa kiangazi wanyama huhangaika sana kupata chakula.
Hata hivyo, anasema kuwa mkulima anaweza kuchukua hatua kwa kuvuna malisho na hatimaye kuyakausha ili yatumike na mifugo wake katika misimu yote bila kutaabika.
Hatua hiyo, anasema inaweza kurahisishwa endapo mkulima anaweza kutenga sehemu maalum ya shamba lake kwa ajili ya kukuza malisho tu.
Hasara ya mvua nyingi
Akilimali imebaini kuwa licha ya mvua nyingi hususan kwenye maeneo ya nyanda za juu, wakulima bado wanapitia changamoto ya ukosefu wa soko la maziwa yao.
Anaungama kuwa muda huu uzalishaji wa maziwa huwa zaidi ya mara mbili ya kiwango cha kawaida kutokana na hali ya malisho kupatikana kwa wingi.
Anasema Kaunti ya Uasin Gishu ni kielelezo cha kaunti nyingi nchini ambazo huzalisha maziwa kwa wingi ila bei ya maziwa haijaimarika.
“Licha ya kwamba serikali kuu imeweka mikakati mingi ili kuhakikisha kuwa kiwango cha uzalishaji maziwa nchini kinapanda, bado hakuna utaratibu wa kuhakikisha kuwa maziwa yanapata soko la uhakika,” anasema.
Ukosefu wa soko tayari umewafanya wakulima wengi kutoka maeneo ya ukanda wa Bonde la Ufa kuwazia aina nyingine ya kilimo kama vile kupanda kahawa au majani chai.
Aidha anasema ingawa ukosefu wa malisho msimu wa kiangazi huathiri shughuli nyingi za ufugaji wa ng’ombe wa maziwa, mambo hubadilika na kuwa mabaya zaidi msimu wa mvua unapowadia.
Ushauri wake ni kuwa ni lazima wakulima wawe na utaratibu wa kuvuna na kuhifadhi malisho msimu wa mvua ili kuwafaa wakati wa kiangazi.
Hatua hii, anasema itawasaidia kutengeneza hela nzuri kibiashara kwa sababu bei ya maziwa huwa imepanda.
Changamoto nyingine ni uhaba wa vifaa vya kusindika maziwa wakati kama huu ambao bidhaa yenyewe inapatikana kwa wingi.
Mitambo inaweza kufaa wakulima hasa wakati wanapozalisha maziwa kwa wingi.
Kuna mitambo ambayo ina uwezo wa kuhifadhi lita nyingi za maziwa yasiharibike haraka, yakisubiri kufikishwa sokoni.
Vifaa hivi hutumika kwa majukumu mengi mojawapo ikiwa ni kupima ubora wa maziwa endapo yatakuwa yameongezewa vitu vingine kama maji ambavyo havistahili.
Aidha pana zana za kuyachanganya, kupakia na namna sahihi ya kupakia kabla ya kuyasafirisha sokoni.