Mfano wa dondoo katika hadithi ‘Harubu ya Maisha’ ndani ya ‘Mapambazuko ya Machweo’
JUMA hili naomba tuangazie mfano wa ku jibu swali la dondoo kati ka diwani ya Mapambazuko ya Machweo na Hadithi Nyingine.
Maagizo:
Isome hadithi husika kisha uyajibu maswali.
“Unalala nini sasa?” Alianza.
“Kwani pana jingine la kufanya ila kulala?” Nilimjibu kwa hasira.
(a) Eleza muktadha wa dondoo hili.
Mama Mercy anamuuliza mumewe Kikwai kwa bezo kama analala. Kikwai anamjibu hapakuwa na jambo la kufanya wakati ule.
Wamo nyumbani mwao. Majibizano haya yanasababishwa na kitendo cha Kikwai kurejea kutoka kazini majira ya usiku bila chakula.
(b) Jadili sifa na umuhimu wa msemaji wa kwanza.
Mama Mercy ni mbishi. Haafiki lolote aambiwalo na Kikwai. Kikwai alimwelezea kuwa hawajapokea mshahara kwa muda wa miezi miwili hivyo hawezi kuikimu familia yake.
Badala ya kumwelewa, alimkaripia.
Mama Mercy ni mwenye mapuuza. Hakujishughulisha kumtafutia mwanao chakula bali anamsubiri Kikwai arejee kutoka kazini ndipo atafute chakula.
Mama Mercy ni mwenye msimamo thabiti. Hapendi kuchukua mikopo. Alihiari kumsubiri Kikwai atoke kazini kuliko kukopa unga dukani.
Umuhimu
Mama Mercy anaendeleza maudhui ya athari ya kazi/ajira katika mshikamano wa jamii.
Wafanyakazi hupitisha muda mwingi ofisini na kukosa muda na familia zao. Kikwai yu ofisini hadi saa nne kasorobo za usiku. Hapati nafasi ya kushinda na familia yake nyumbani.
Mtagusano kati yake na Kikwai unamulika sifa ya Kikwai kama mwajibikaji. Kikwai anajitahidi kumtafutia Mercy chakula japo hana hela.
Anakopa chakula kwa duka na kuomba usaidizi kutoka kwa Bishop wao.
Mama Mercy anasawiri mbinu-ishi ya kujithamini. Anajitenga na udaku. Vaite anamheshimu kati ya wanawake wanaoishi katika mtaa wao kwa sababu ya kutoshiriki katika vikao vya masengenyo.
Mama Mercy ni mfano wa wanawake wanaowatweza waume zao. Alimgombeza Kikwai kwa kutoweza kuilisha familia yake akisema wangekufa njaa.
(c) Tambua mbinu ya mtindo iliyotumika katika dondoo
Swali la balagha – Unalala nini sasa?
(d) Eleza dhima ya mbinu hii katika maandishi
Hutumiwa kuwasuta watu wanapokosa kutimiza matarajio ya watu katika jamii. Mama Mercy anamzoma mumewe kwa kumuuliza alichopika ilhali alifahamu hapakuwa na chakula mle nyumbani.
“Ningepika nini?” (uk. 26)
Maswali ya balagha huulizwa kusisitiza jambo. Mama Mercy hakuelewa ni vipi mtu anaweza kufanya kazi na akose kufidiwa kwa jasho lake.
“Kila siku hatu jalipwa… Mpaka lini? Mbona sikuelewi?’ (uk. 27)
Maswali haya hutumiwa kumzindua msomaji adadisi jambo. Kikwai aliwaza ni vi pi Vaite alikuja kujua kwamba Mama Mercy hashiriki umbeya.
Ni ishara kuwa Vaite huchangia maongezi haya. ‘Amejuaje hilo?’ (uk. 26).