Habari

Ruto atia saini sheria za kahawa, hali ya hewa na miundombinu

Na SAMWEL OWINO March 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI sasa inaweza kutumia hadi asilimia 90 ya fedha zinazokusanywa kupitia Ushuru wa Maendeleo ya Reli kupata ufadhili wa ziada kwa miradi ya miundombinu ya reli baada ya Rais William Ruto kutia saini kuwa sheria Mswada wa Marekebisho ya Ada na Ushuru Mbalimbali.
Rais alitia saini mswada huo pamoja na miswada mingine miwili — Mswada wa Kahawa wa 2023 na Mswada wa Hali ya Hewa wa 2023 — katika Ikulu siku ya Ijumaa asubuhi, Machi 13.
Katika sekta ya kilimo, Rais Ruto pia alitia saini Mswada wa Kahawa wa 2023 kuwa sheria, hatua inayolenga kufanya mageuzi makubwa katika usimamizi wa sekta ya kahawa nchini.
Mswada huo uliodhaminiwa na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa, Kimani Ichung’wah pamoja na Seneta wa Kirinyaga, James Murango, unapendekeza kuhamisha majukumu ya udhibiti na biashara ya kahawa kutoka kwa Mamlaka ya Kilimo na Chakula (AFA) kwenda Bodi ya Kahawa ya Kenya.
Wakati huo huo, Rais pia alitia saini Mswada wa Hali ya Hewa wa 2023, ambao sasa utaanzisha Mamlaka ya Huduma za Hali ya Hewa Kenya.
Mamlaka hiyo itakuwa mshauri mkuu wa kiufundi kwa serikali ya kitaifa na serikali za kaunti kuhusu masuala ya hali ya hewa.